Ticker

6/recent/ticker-posts

WAZIRI MKUU AZINDUA TAWI LA BENKI YA MWANGA NA KUTOA MAAGIZO SABA



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezindua tawi la benki ya Mwanga Hakika jijini Dodoma na kuitaka benki hiyo iwe kimbilio la wajasiriamali na wakulima wadogo.



“Kuweni kimbilio la wajasiriamali na wakulima wadogo. Njooni na bidhaa na vivutio muhimu kwa makundi hayo ya wajasiriamali na wakulima wadogo. Hilo ni kundi ambalo linahitaji zaidi huduma zenu katika kuliwezesha kujikwamua kiuchumi,” amesema.



Ametoa wito huo leo (Jumanne, Agosti 31, 2021) wakati akizungumza na viongozi mbalimbali, wanahisa na wananchi waliohudhuria uzinduzi wa tawi la benki ya Mwanga Hakika (Mwanga Hakika Bank) jijini Dodoma.



Waziri Mkuu ameitaka benki hiyo ipunguze riba ili kuendana na dhamira ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye amekuwa akilisemea suala hilo mara kwa mara. “Nanyi pia lizingatieni hili katika kukua kwenu kwani kupungua kwa kiwango cha riba kutasaidia kusisimua biashara na shughuli nyingine za kiuchumi,” amesisitiza.



Ameitaka benki hiyo iongeze ubunifu. “Kuweni wabunifu. Sambamba na kutengeza faida, kuongeza amana za benki na kutoa gawio kwa wanahisa, njooni na ubunifu utakaoboresha huduma zenu na kuzifanya kuwa ubora zaidi, zenye tija na gharama nafuu kwa walaji.”



Ameitaka benki hiyo ipunguze gharama za tozo kwani tozo za mabenki kwa wateja bado ni kubwa na wakati mwingine haziendani hata na mfumuko wa bei. “Hakikisheni huduma za kibenki zisiwe kikwazo kwa wananchi wa kawaida.”



“Sogezeni huduma kwa wananchi hususan maeneo ya pembezoni ili kuwahakikishia usalama wao pamoja na fedha zao. Angalieni uwezekano wa kufungua matawi huko Mpwapwa, Kongwa, Kondoa, Bahi na maeneo mengine ya jirani ikiwa ni njia ya kupanua wigo kwa kuwafuata wateja.”



Amesema MHB hawana budi kuimarisha utoaji wa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa kuwa na akaunti sambamba na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wateja. “Waelimisheni wananchi ili waache kutunza fedha majumbani, wekeni matawi madogo madogo ili wafungue akaunti kwa urahisi,” amesisitiza.



Waziri Mkuu ameitaka benki hiyo iunge mkono juhudi za Serikali ili kuwezesha kufikiwa kwa azma ya Serikali kujenga uchumi wa viwanda. “Iungeni mkono Serikali hii kwa kukuza kilimo, viwanda na biashara. Tuwaondoe wananchi woga wa kukopa katika benki. Mheshimiwa Rais amekuwa akihamasisha watu wafanye biashara na lengo la Serikali hii likiwa ni kutoka katika uchumi wa kati ulio chini na kwenda katika uchumi wa kati ulio juu,” amesema.



Amesema benki ndicho chombo kikuu cha kutolea huduma za kifedha kwa wananchi. Hivyo, katika kuwahudumia wananchi wazingatie mahitaji yao, wawahamasishe na kuwaelimisha umuhimu wa kutumia benki.



Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na hadhara iliyokuwepo, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa aliwapongeza wanahisa wa MHB kwa uamuzi wao wa kuunganisha taasisi tatu za kifedha na kufikia kuwa benki inayotoa huduma tofauti na hapo awali.



Waziri Bashungwa ambaye alizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha, alisema benki hiyo imeweza kuwafikia wateja zaidi ya 100,000 na kutoa mikopo ya sh. bilioni 38.9 baada ya kuunganisha taasisi za kibenki za EFC Tanzania Microfinance Bank (EFC), Hakika Microfinance Bank (Hakika) na Mwanga Community Bank (MCB).



“Tunataraji kuwa mikopo hii itakuwa na manufaa kwa sekta mbalimbali za kiuchumi na nipende kuwahakikishia uongozi wa Mwanga Hakika Bank kuwa itapata ushirikiano kutoka Serikalini,” alisema.



Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo, Prof. Adolf Mkenda aliiomba benki hiyo iwasaidie wakulima hasa kwenye mazao ya alizeti na zabibu ambayo ni maarufu mkoani Dodoma na Serikali imeamua kuyatilia mkazo ili kuongeza uzalishaji wake.



“Tunahitaji wafanyabishara kwenye sekta ya kilimo kama vile wanunuzi wa mbolea na viuatilifu. Tunahitaji watu wa kusindika mazao ya wakulima (agro-processing) na wasambazaji wa viuatilifu (agro-chemicals). Ninaahidi kufanya kazi kwa ukaribu na Mwanga Hakika Bank ili kuinua kilimo,” alisema.



Naye, Naibu Gavana wa Benki Kuu, Dkt. Bernard Kibesse alisema uzinduzi wa tawi hilo jijini Dodoma, utahakikisha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi (financial inclusion) na kwamba uamuzi wa kuunganisha taasisi tatu umewawezesha kuwa na mtaji mkubwa zaidi.



“Miaka michache iliyopita taasisi hizo zilikuwa zinatishiwa kufungwa na Benki Kuu kwa kukosa mtaji wa shilingi bilioni mbili. Leo hii wamevuka lengo la sh. bilioni 15 zinazotakiwa ili waweze kuwa benki ya kibiashara. Kwa hiyo, waje wakati wowote ili wakamilishe taratibu na tuwape kibali hicho,” alisema.


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza wakati alipozindua Tawi la Benki ya Mwanga Hakiki jijini Dodoma, Agosti 31, 2021.(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)




Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Dkt Benard Kibessa (kulia) na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Bodi ya Benki ya Mwanga Hakika, Ridhiwani Mringo tawi la Dodoma, baada ya kuzindua tawi hilo Agosti 31, 2021.Kushoto ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa katika picha ya pamoja na viongozi pamoja na watumishi wa Benki ya Mwanga Hakika baada ya kuzindua tawi la Benki hiyo jijini Dodoma, Agosti 31, 2021. Waliokaa kutoka kushoto ni Waziri wa Kilimo, Profesa Adolf Mkenda, Naibu Spika wa Bunge, Dkt. Tulia Ackson, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki hiyo, Ridhiwani Mringo, Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Dkt. Benard Kibessa na kulia ni Waziri wa Viwanda na Biashara, Profesa Kitila Mkumbo.. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizindua Tawi la Benki ya Mwanga Hakika jijini Dodoma, Agosti 31, 2021. Wengine pichani kutoka kushoto ni Waziri wa Kilimo, Profesa Adolf Mkenda, Waziri wa Viwanda na Biashara, Profesa Kitila Mkumbo, Naibu Spika wa Bunge, Dkt. Tulia Ackson, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki hiyo, Ridhiwani Mringo, Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Dkt. Benard Kibessa na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo Jagjit Singh. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Post a Comment

0 Comments