Ticker

6/recent/ticker-posts

SIMAMIENI VIZURI FEDHA ZA HALMASHAURI-MAJALIWA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza wakati alipofungua Mafunzo kwa Waheshimiwa Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri nchini kwenye ukumbi wa Mabeyo Complex jijini Dodoma, Juni 28, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiagana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Innocent Bashungwa (wa pili kulia), Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka (kulia), Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara) Christina Mndeme (wa pili kulia), Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa (ALAT), Mushid Ngeze (wa tatu kushoto) na Katibu Mkuu wa ALAT, Elirehema Kaaya, baada ya kufungua Mafunzo kwa Waheshimiwa Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri kwenye ukumbi wa Mabeyo Complex jijini Dodoma, Juni 28, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Innocent Bashungwa (wa tatu kulia), Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka (kulia) na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Mushid Ngeze wakiimba Wimbo wa Taifa wakati Waziri Mkuu alipofungua Mafunzo kwa Waheshimiwa Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri kwenye ukumbi wa Mabeyo Complex jijini Dodoma, Juni 28, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Innocent Bashungwa akizungumza wakati alipomkaribisha Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akufungua Mafunzo kwa Waheshimiwa Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri kwenye ukumbi wa Mabeyo Complex jijini Dodoma, Juni 28, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

***********************

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri wasimamie ipasavyo matumizi ya fedha zilizokusanywa na zile zinazotoka Serikali Kuu na wahakikishe zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Ameyasema hayo leo (Jumanne, Juni 28, 2022) wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri wa Tanzania Bara katika ukumbi wa Mabeyo Complex jijini Dodoma. Amesema lazima viongozi wajue fedha zinazoingia na maelekezo yake.

Amesema Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa kila mwaka inaibua makosa yale yale ikiwamo kuhamisha fedha kutoka fungu moja kwenda jingine bila kufuata taratibu zilizowekwa na kufanyika kwa malipo bila ya kuwepo maelezo au vielelezo.

“Fedha za makusanyo kutumika kabla ya kupelekwa benki. Lazima muhoji kwa nini na mjue hilo haraka. Pia mjiridhishe pale wanaposema hakuna mtandao je ni kweli hakukuwa na mtandao. Fuatilieni na ununuzi wa vifaa hewa hasa kipindi hiki cha ujenzi wa miradi.”

“Viongozi wote mlioshiriki mafunzo mkasimamie vema utawala bora na utawala wa sheria ikiwa ni pamoja na kuimarisha mfumo wa utatuzi wa migogoro sambamba na ushirikishaji wananchi katika maamuzi na mipango ya maendeleo.”

Mheshimiwa Majaliwa amesema viongozi wote wanatakiwa wahakikishe wananchi wanapata taarifa za utekelezaji wa mipango na bajeti za kutekeleza mipango hiyo. “Utoaji wa taarifa za mapato na matumizi ni muhimu katika kujenga imani kwa wananchi.”

Waziri Mkuu amewataka viongozi hao waimarishe usimamizi wa miradi ya maendeleo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kazi zinazofanywa zilingane na fedha inayotumika. “Kasimamieni viwango vya ubora wa miradi inayotekelezwa na utekelezaji wa makubaliano yaliopo kwenye mikataba.”

Kwa uapnde wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Innocent Bashungwa amesema mafunzo hayo ya siku mbili yameandaliwa kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kusimamia uendeshaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mameya wa Halmashauri za Majiji na Manispaa na Wenyeviti wa Halmashauri za Wilaya na Miji.

Post a Comment

0 Comments