Ticker

6/recent/ticker-posts

RC BABU KUFUNGUA TAMASHA LA JINSIA KANDA YA KASKAZINI OKTOBA 5 VIWANJA VYA KWASA KWASA SAME


Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi akitoa tamko kuhusu Tamasha la Jinsia mwaka 2022 Kanda ya Kaskazini litakalofanyika wilayani Same kuanzia Oktoba 5-7,2022. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkuu wa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Mhe. Edward Mpogolo akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini litakalofanyika katika viwanja vya Kwasa Kwasa wilayani Same. 
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi akitoa tamko kuhusu Tamasha la Jinsia mwaka 2022 Kanda ya Kaskazini litakalofanyika wilayani Same kuanzia Oktoba 5-7,2022. 

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog SAME

Zaidi ya wadau 500 wanaotetea haki za wanawake na usawa wa jinsia na wanaharakati binafsi wanatarajiwa kushiriki katika Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini litakalofanyika kuanzia Oktoba 5 hadi 7,2022 katika viwanja vya Kwasa Kwasa Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro.


Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Jumanne Oktoba 4,2022 katika ukumbi wa Elephant Motel wilayani Same, Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi amesema Tamasha hilo limeandaliwa na TGNP kwa kushirikiana na wadau wanaotetea haki za wanawake na usawa wa jinsia na wanaharakati binafsi kwa ufadhili wa Ubalozi wa Watu wa Canada, Sweeden, Coady Institute Canada na Seedchange.

Liundi amesema Tamasha la Jinsia 2022 linalotarajiwa kufunguliwa rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Babu litatoa fursa ya kutafakari na kutathmini changamoto zilizopo na namna kuweka mikakati ya kukabiliana na changamoto hizo likiongozwa na mada kuu isemayo, ‘Haki ya Uchumi: Rasilimali Ziwanufaishe Wananchi Walioko Pembezoni kwa Maisha Endelevu’.

“Pia kutakuwa na mada ndogo ndogo ambazo ni pamoja na Haki za Uchumi: Wezesha fursa za kilimo kuwanufaisha makundi yaliyopembezoni kwa Maisha Endelevu, Uongozi Shirikishi, chachu ya haki za kiuchumi na maendeleo endelevu, Mila kandamizi kikwazo cha haki za uchumi kwa maendeleo endelevu, Boresha upatikanaji wa huduma za jamii ili kuwezesha upatikanaji wa huduma za afya ya uzazi kwa wote na Harakati za Ujenzi wa Nguvu za Pamoja -Tapo: Msingi wa maendeleo jumuishi na endelevu kwa wote”,ameeleza Liundi.


Akifafanua zaidi, Liundi amesema Tamasha hilo litahusisha mawasilisho, mijadala ya pamoja, maonesho na warsha ambapo Mijadala ya pamoja itajenga dhana halisi kuhusu mada ndogo katika siku husika.

“Siku ya mwisho  ya Tamasha Oktoba 7,2022 itahusisha kufunga kwa kuyaweka pamoja masula yaliyoibuka katika mijadala mbalimbali siku zote tatu za Tamasha. Kwa kuzingatia masuala yaliyoibuliwa, washiriki watatengeneza mipango mkakati kwa ajili ya utekelezaji”,amesema.


“Maonesho yatafanyika katika siku zote za Tamasha kutoa nafasi kwa mashirika na mitandao inayoshiriki kuonesha kazi zao kupitia njia mbalimbali kama vile video, mabango, picha n.k. Wachapishaji, AZAKI na wanawake binafsi pia wanakaribishwa kuonesha na kuuza bidhaa zao. 

Sehemu maalumu zitatolewa kwa vikundi maalum kutengeneza vitovu vya mtandao, kupeana taarifa na kupanga mikakati ya pamoja”,ameongeza Liundi.

Akizungumza na Waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Mhe. Edward Mpogolo ameushukuru Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kupeleka Tamasha la Jinsia katika wilaya ya Same akibainisha kuwa tamasha hilo litaleta fursa kubwa kiuchumi.

“Tunawashukuru sana TGNP kwa maamuzi mazuri ya kufanyia Tamasha la Jinsia katika wilaya ya Same, tunaamini kabisa mara baada ya tamasha hili kutakuwa na mabadiliko makubwa kwa wananchi kwani tamasha lina fursa mbalimbali. Tamasha hili litakuwa darasa kubwa sana kwetu kiuchumi. Karibuni sana”,amesema Mpogolo.

“Tutajifunza kupitia kwa wageni tutakaowapokea nanyi mtajifunza pia kupitia kwetu. Sisi hapa tunalima sana zao la Tangawizi lakini pia tunalima mpunga, nyanya na vitunguu hivyo kupitia tamasha hili pia tutapata fursa za namna ya kuboresha kilimo chetu ili kiwe na tija zaidi”,ameeleza.


Mkuu huyo wa wilaya ya Same ametumia fursa hiyo kuwahakikishia washiriki wa tamasha hilo ulinzi na usalama wa kutosha katika kipindi chote cha tamasha la jinsia Kanda ya Kaskazini.

“Wilaya ya Same ipo salama, napenda kuwahakikishia kuwa ulinzi na usalama utakuwepo, hatutapenda kuona mgeni anadhurika au kuibiwa. Hapa Same hatujawahi kuwa na wageni zaidi ya 500, hii ni bahati ya pekee sana tunawahakikishia kuwa wageni wetu watakuwa salama muda wote”,amesema Mpogolo.


Tamasha la Jinsia ni moja ya majukwaa ya TGNP katika ujenzi wa nguvu za Pamoja. 

Jukwaa hili ni la wazi kwa ajili ya wanawake na wadau wa haki za binadamu ambao hukutana pamoja kila baada ya mwaka mmoja kubadilishana uzoefu, kusherehekea, kutathmini na kupanga mipango ya kukabiliana na changamoto zinazowakabili.

TGNP iliratibu tamasha la kwanza kabisa mwaka 1996 na hadi sasa takribani matamasha 14 yamekwishafanyika ambapo yameweza kuleta pamoja zaidi ya washiriki 25,000 (70% wanawake na 30%wanaume) katika viwanja vya TGNP.


Kutokana na mafanikio ya Tamasha kubwa la Jinsia, mwaka 2010, TGNP na washirika wake walizindua tamasha la jinsia la kwanza ngazi ya wilaya ambapo hadi sasa matamasha sita ya Jinsia yamefanyika katika ngazi ya wilaya na kuleta pamoja zaidi ya washiriki 6000 (70% wanawake and 30% wanaume).

 Tamasha la kwanza ngazi ya Wilaya lilifanyika Kisarawe (2010), likafuatiwa na Mkambarani, Morogoro (2012), Tarime (2014), Mkambarani  Morogoro (2016), Kishapu Shinyanga (2018) na Mbeya (2020).


Kama sehemu ya kuendelea kutanua hatakati za ujenzi wa nguvu za pamoja nchini na kutoa fursa kwa watu wengi zaidi kushiriki, ilionekana kuna uhitaji wa kuanzisha Tamasha la Jinsia katika ngazi ya Kanda ambalo litaleta pamoja washiriki toka kanda mbalimbali hapa nchini.


TGNP ni shirika lisilo la kiserikali lilioanzishwa mwaka 1993.

 Katika miaka ya hivi karibuni, TGNP imetoa mchango mkubwa katika kukuza mashirikiano ya asasi za kiraia kwa kujenga uwezo wa kuchanganua na kuibua mijadala ya umma na hivyo kuleta mapinduzi ya kijinsia na hatua za pamoja kwenye masuala muhimu ya maendeleo kijamii, kiutamaduni, kisiasa na kiuchumi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi akitoa tamko kuhusu Tamasha la Jinsia mwaka 2022 Kanda ya Kaskazini litakalofanyika wilayani Same kuanzia Oktoba 5-7,2022. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi akitoa tamko kuhusu Tamasha la Jinsia mwaka 2022 Kanda ya Kaskazini litakalofanyika wilayani Same kuanzia Oktoba 5-7,2022.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi akitoa tamko kuhusu Tamasha la Jinsia mwaka 2022 Kanda ya Kaskazini litakalofanyika wilayani Same kuanzia Oktoba 5-7,2022.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi akitoa tamko kuhusu Tamasha la Jinsia mwaka 2022 Kanda ya Kaskazini litakalofanyika wilayani Same kuanzia Oktoba 5-7,2022.
Mkuu wa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Mhe. Edward Mpogolo akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini litakalofanyika katika viwanja vya Kwasa Kwasa wilayani Same.
Mkuu wa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Mhe. Edward Mpogolo akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini litakalofanyika katika viwanja vya Kwasa Kwasa wilayani Same.
Mkuu wa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Mhe. Edward Mpogolo akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu Tamasha la Jinsia Kanda ya Kaskazini litakalofanyika katika viwanja vya Kwasa Kwasa wilayani Same. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi.
Mkuu wa wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Mhe. Edward Mpogolo akipiga picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi (kulia) na Meneja Mradi wa Coady Institute Canada, Bw. Eric Smith (kushoto).

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Post a Comment

0 Comments