Ticker

6/recent/ticker-posts

BARABARA YA BUGENE-BURIGI CHATO IKAMILIKE KWA MUDA ULIOPANGWA KUFANYA KAZI NDANI YA MUDA ALIOPEWA



*********************

Na Shemsa Mussa, KAGERA.


Katika ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Mhe. Albert John Chalamila Ndani ya Wilaya Karagwe amemtaka mkandarasi wa barabara ya Bugene hadi Burigi Chato kufanya kazi ndani ya muda uliyopo kwenye mkataba na kumaliza kazi kwa wakati.


Akizungumza mara baada ya kukagua barabara hiyo yenye kilometa 60 amemtaka msimamizi wa mradi huo, Tanroad Engneering Consultanting Unit (TECU) kumsimamia mkandarasi huyo ili afanye kazi ndani ya muda aliopewa katika mkataba kwani lengo la Mheshimiwa Rais ni kuleta fedha kwa wananchi na kuhakikisha fedha hizo zinafanya kazi kwa muda uliokusudiwa ili wananchi wapate maendeleo.


“Hii ni barabara ya kilometa 120 ila mpaka sasa wameanza na kilometa 60, barabara hii itakuwa na gharama ya jumla ya Tshs. bilioni 109 na inatakiwa ikamilike ndani ya muda wa miezi 30. Mpaka sasa mkandarasi ameshatumia miezi saba na mkandarasi yupo nyuma kidogo ya asilimia alizotakiwa kuwa amefanya kazi, hivyo sisi tunamsisitiza aongeze kasi ili kuendana na muda aliopewa,” ameeleza Mhe. Chalamila


Sambamba na hayo ameielekeza Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Karagwe kuwawajibisha baadhi ya watu wanaoiba vifaa vya ujenzi wa barabara hiyo na kutoa onyo tabia hiyo ya wizi isijirudie tena. Pia amemtaka Meneja wa Tanroad na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Karagwe kuwakamata na kuwafikisha mahakamani watu wote wanaochimba mchanga eneo la hifadhi ya barabara kwani unapoweka mitaro ambayo haihusiki kwenye barabara unaongeza gharama na kuhatarisha usalama wa maisha ya watu. Lakini pia kwa mashimo wanayochimba yanaacha mapango ambayo yanachochea ufiche wa majambazi hivyo kutengeneza barabara ambayo haina usalama.


"Hatuwezi kufanya kazi na wezi maendeleo yakawepo na tabia hii ikomeshwe mapema sana na wale mnaochimba mchanaga dawa inachemshwa jueni mnaharibu barabara lakini hayo mapango zinaweza kuwa nyumba za majambazi " amesema Chalamila.


Aidha, kwa wale ambao makazi yao yanapaswa kuondolewa, nyumba zao waziondoe haraka ili ujenzi wa barabara hiyo usiweze kukwama na kukamilika kwa wakati kwani nia ya Serikali ni kutekeleza mradi ndani ya muda na kwa kufanya hivyo kunaweza kuufanya Mkoa kupata miradi mingine zaidi.


Barabara inayojengwa ya Bugene hadi Burigi Chato ni kilometa 60 inajengwa na mkandarasi kutoka China Road and Bridge Cooperation (CRBC) ya Jijini Dar es salaam chini ya usimamizi wa Tanroad Engneering Consultanting Unit (TECU) kwa gharama ya Tsh. bilioni 109 pamoja na VAT.

Post a Comment

0 Comments