Ticker

6/recent/ticker-posts

KONGAMANO LA KIMATAIFA LA MABADILIKO YA TABIA KUFANYIKA NCHINI OKTOBA 2023



************

Tanzania itakuwa mwenyeji wa Kongamano la Kimataifa la Vijana na Mabadiliko ya Tabianchi 2023 na kuwakutanisha washiriki zaidi ya 500 kutoka nchi mbalimbali Duniani.

Kongamano hilo linaloandaliwa kwa ushirikiano baina ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania- TFS na Global Youth Leadership Center - GYLC ya Marekani, litawakutanisha washiriki 200 ana kwa ana huku zaidi wa washiriki 300 kutoka nchi zaidi ya 50 wakishiriki mtandaoni.

Akizungumzia mkutano huo, Mratibu mwendeshaji wa mkutano huo na Mkurugenzi wa GYLC, Ejaj Ahamad, alisema mkutano huo utakuwa ni wa siku tatu na unatarajiwa kuanza Oktoba, 2023 katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam 

Alisema katika Kongamano hilo siku ya kwanza itahusisha kikao huku siku ya pili na tatu zikihusisha shughuli mbalimbali zinazolenga kuonyesha kwa vitendo jitihada za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kama vile kupanda miti.

"Kongamano hili mwaka jana lilifanyika nchini India lakini mwaka huu nimeamua kulifanyia nchini Tanzania baada ya kuvutiwa na jitihada za uhifadhi nilizozifahamu kupitia Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi (COP27) uliofanyika Misiri Mwaka jana,” alisema Ahmad.

Aliongeza kuwa yupo nchini kwa ajili ya maandalizi ambapo atatumia uwepo wake kukutana na wadau mbalimbali ikiwemo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira.

Kamishna wa Uhifadhi TFS, anasema kufanyika kwa Global Climate Summit 2023 nchini Tanzania kwa mara ya kwanza kutaleta neema kwa kuimarisha shughuli za uhifadhi, kukuza sekta ya utalii hususani katika maeneo yaliohifadhiwa na kukuza biashara kutokana na mkusanyiko mkubwa wa watu kutoka nchi tofauti.

Post a Comment

0 Comments