Ticker

6/recent/ticker-posts

PUMA ENERGY TANZANIA YASEMA HAINA UHABA WA MAFUTA

Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Puma Energy Tanzania imesema kwa upande wake haina changamoto ya uhaba wa mafuta na kwamba mahitaji ya nishati hiyo yamezidi kuongezeka.

Imesema Agosti mwaka huu kampuni hiyo inatarajia kutapata mafuta ya dizeli na petroli lita zaidi ya milioni 60, hivyo imewatoe hofu wauzaji wakubwa na wadogo kuhusu hofu ya bidhaa hiyo.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji Kampuni ya Puma Energy, Fatma Abdallah mbele ya Waziri wa Nishati January Makamba ambaye alifika kwenye tanki za kuhifadhia mafuta za kampuni hiyo ambapo amesema kwa Julai kumekuwa na mahitaji makubwa ya mafuta huku akieleza katika iliyoisha jana wameuza petroli na dizeli lita zaidi ya milioni 36.

Amesema hali hiyo ni tofauti na mwaka 2022 waliuza milioni 30. Hata hivyo, amewatoa hofu Watanzania akiwaeleza kuwa mafuta yapo ya kutosha.

Aidha amesema wanatarajia kuuza zaidi ya lita milioni 50 za mafuta hadi mwezi huu unaisha." Tunauza mafuta yetu kwa wateja wakubwa wadogo, meli zinazokuja pia zina mzigo wetu na kabla ya Julai haijaisha tunatarajia kupata lita milioni 16.

“Agosti tutapata mafuta ya dizeli na petroli lita zaidi ya milioni 60, niwatoe hofu wauzaji wakubwa na wadogo mafuta yapo ya kutosha na tunashirikiana kwa ukaribu na Serikali.," amesema.

Kuhusu changamoto inayowakabili Mkurugenzi Mtendaji Fatma amesema kwa sasa ni upungufu wa dola za Marekani ambapo ameiomba Serikali kuangalia namna ya kusaidia upatikanaji wa fedha hizo. “Tunaomba tupate dola za Marekani za kutosha zitakazotusaidia kuagiza mafuta ya kutosha na kuyafikisha Tanzania."

Akipokea changamoto hiyo Waziri wa Nishati January Makamba amewahakikishia wadau mbalimbali akiwemo Fatma na kampuni yake kwamba Serikali inatambua changamoto hiyo, inaifanyia kazi kwa ukaribu.

Waziri Makamba amewatoa wasiwasi wadau hao na kusisitiza kuwa Serikali imeipokea changamoto hiyo.
Waziri wa Nishati January Makamba( wa pili kulia) akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mafuta ya Puma Tanzania Fatma Abdallah(kushoto) baada ya Waziri kutembelea katika eneo la kuhifadhia mafuta ya kampuni hiyo

Post a Comment

0 Comments