Ticker

6/recent/ticker-posts

MCHENGERWA - TAMASHA LA BIBI TITI KUFANYIKA WIKI NZIMA, KUELEZEA MAFANIKIO YA SERIKALI



Na John Mapepele

Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa (MNEC) CCM kupitia Mkoa wa Pwani ambaye na Waziri wa Maliasili na Utalii ambaye pia ni Mbunge wa Rufiji, Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema tamasha la tatu la kumbukizi ya Bibi Titi Mohamed litafanyika Disemba mwaka huu likiwa na lengo la kumuenzi na kuonyesha mapinduzi yanayofanywa na Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha uchumi na kuwaletea maendeleo wananchi.

Mhe. Mchengerwa ametoa Kauli hiyo leo Ikwiriri – Rufiji na Kibiti kwenye mikutano ya CCM wakati akimkaribisha Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Pwani, Mwishehe Ramadhan Mlao kuwahutubia wana CCM. Mikutano hiyo ni mahsusi kwa ajili ya kuwashukuru wana CCM kwa kuwachagua viongozi mbalimbali wa CCM katika uchaguzi uliopita.

Amefafanua kuwa Tamasha la mwaka huu litakuwa tofauti na la awali na kwamba litaadhimishwa kwa wiki nzima huku shughuli za maonesho ya mafanikio ya maendeleo yaliyofanywa na Serikali katika kipindi hiki kwa nyanja mbalimbali yakionyeshwa.
Aidha, wasanii nguli watatumbuiza ikiwa ni pamoja na wasanii wa Rufiji kutengewa siku nzima ili kuwaburudisha wananchi ambapo maonesho hayo yataonyeshwa mubashara katika mitandao mbalimbali duniani.

Amewataka wananchi kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa aliyoifanya katika kipindi kifupi huku akiwasihi kupuuza baadhi ya mitandao inayoeneza uzushi wa kupinga maendeleo yanayofanywa na Serikali ikiwa ni pamoja na suala la Bandari.


“Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa ya kuwaletea maendeleo wananchi, lakini kuna baadhi ya watu wanaweka propaganda zao kwenye mitandao, tunatakiwa kuwakataa na kuwakemea watu hao kwa kuwa nia yao siyo njema wanataka kushika dola na siyo kuwasaidia wananchi.”Amesisitiza Mhe. Mchengerwa

Ameyataja baadhi ya mafanikio yaliyopatikana katika kipindi hiki kwa Wilaya ya Rufiji kuwa ni pamoja na kwa ujenzi wa Shule, Zahanati, madaraja, barabara na viwanja vya michezo.

Amewataka wananchi wa Rufiji kufanya kazi kwa bidii ili kuunga mkono juhudi za Serikali za kuimarisha uchumi na kuendelee kuenzi bibi Titi ambaye amemwelezea kuwa ni shujaa aliyekuwa anaamini katika kufanya kazi.
Naye Mwenyekiti Mlao amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwaletea maendeleo wananchi huku akiwataka wanaCCM kufanya kazi, kuwa na umoja huku wakilinda amani iliyoachwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, huku pia akimpongeza Mhe. Mchengerwa kwa kazi kubwa anaoyoifanya ya kuwaletea wananchi wa Rufiji maendeleo.

Katika mkutano huo wanaCCM wamempatia Mwenyekiti zawadi ya Mbuzi na kumvisha shuka la kimasai ikiwa ni ishara ya kumheshimu kiongozi huyo wa Mkoa.



Post a Comment

0 Comments