Ticker

6/recent/ticker-posts

TEKNOLOJIA YA 5G ITARAHISISHA UTOAJI WA HUDUMA - SAMIA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kuhakikisha mifumo yote ya TEHAMA inasomana na taasisi zinazosimamia sera hizo.

Rais Samia ametoa agizo hilo wakati wa uzinduzi wa mkongo wa mawasiliano wa 2Afrika na matumizi ya teknolojia ya 5G iliyofanyika katika ofisi za kampuni ya Airtel zilizopo Tanki Bovu.

Aidha, Rais Samia amesema misingi imara kwenye TEHAMA na mifumo ya mawasiliano kisera, kisheria na kitaasisi itawezesha kujenga uchumi jumuishi wa kidijitali (Digital Inclusive Economy) na kuinua maisha ya wananchi mijini na vijijini.

Vile vile, Rais Samia amesema uzinduzi wa teknolojia ya 5G itarahisisha utoaji wa huduma mbalimbali, ikiwemo utunzaji taarifa muhimu, ukusanyaji maduhuli ya serikali, kutuma na kupokea fedha pamoja na biashara za mitandaoni.

Kwa upande mwingine, Rais Samia amesema kuongezeka kwa mkongo huu kutatoa fursa kwa mitandao ya simu na watoa huduma wengine kuchagua mkongo wanaotaka kutumia, hivyo kuongeza ubora na kushusha gharama za intaneti.

Mkongo wa 2Afrika unaunganisha bara la Asia, Ulaya na Afrika kwa urefu wa kilometa 45,000 na kutumiwa na zaidi ya watu bilioni 3 duniani.

Serikali imeanza mradi wa ujenzi wa minara mipya 758 kwa ajili ya kupanua wigo wa mawasiliano (coverage) itakayowanufaisha Watanzania zaidi ya milioni 8 kote nchini na kupunguza gharama za kuweka mkongo kwenye hifadhi za barabara.

Zuhura Yunus
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akivuta kitambaa kuashiria uzinduzi wa Kituo cha Mkongo wa Baharini cha Airtel 2Afrika kilichopo Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023. Wengine pichani ni Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila, Mtendaji Mkuu wa Kundi la Makampuni ya Airtel Afrika Dkt. Olusegun Ogunsanya, Mtendaji Mkuu wa Airtel Tanzania Dinesh Balsingh pamoja na viongozi wengine wakishuhudia.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa amevaa Kifaa Maalum cha kumuwezesha kuona kwa ukaribu matukio mbalimbali Duniani kijulikanacho kama Teknolojia Ukweli Halisi (Virtual Reality Device) mara baada ya kuwasili katika Kituo cha Mkongo wa Mawasiliano Baharini cha Kampuni ya Airtel Tanzania kilichopo Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023. Wengine katika picha ni Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Nnauye pamoja na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mawasiliano na Simu za Mkononi ya Airtel Tanzania Dinesh Balsingh wakishuhudia tukio hilo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa pamoja na viongozi wengine wakati akimsikiliza Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Nnauye kuhusu Mkongo wa Mawasiliano wa Baharini wa 2Afrika kabla ya kuuzindua katika Kituo hicho cha Kampuni ya Mawasiliano na Simu za Mkononi ya Airtel Tanzania kilichopo Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Nnauye wakati akielekea kuzindua Kituo cha Mkongo wa Baharini cha Airtel 2Afrika cha Kampuni Mawasiliano na Simu za mkononi ya Artel Tanzania kilichopo Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akibonyeza Kitufe kuashiria uzinduzi wa Mtandao wenye kasi ya 5G wa Kampuni ya Airtel Tanzania katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mkongo wa Mawasiliano Baharini cha Kampuni ya Airtel Tanzania kilichopo Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023.
Viongozi mbalimbali wa Serikali na Sekta Binafsi wakiwa kwenye hafla ya uzinduzi wa Kituo cha Mkongo wa Baharini cha Airtel 2Afrika pamoja na Mtandao wenye kasi ya 5G wa Kampuni ya Mawasiliano ya Airtel Tanzania iliyofanyika Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Nnauye wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kituo cha Mkongo wa Baharini cha Airtel 2Afrika pamoja na Mtandao wenye kasi ya 5G wa Kampuni ya Mawasiliano ya Airtel Tanzania iliyofanyika Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali pamoja na wadau wa Mawasiliano kwenye hafla ya uzinduzi wa Kituo cha Mkongo wa Baharini cha Airtel 2Afrika pamoja na Mtandao wenye kasi ya 5G wa Kampuni ya Mawasiliano ya Artel Tanzania iliyofanyika Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisikiliza maelezo kuhusu Kituo cha Mkongo wa Baharini cha Airtel 2Afrika kabla ya kukizindua rasmi kwenye hafla iliyofanyika Mbezi Tanki Bovu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Agosti, 2023

Post a Comment

0 Comments