Ticker

6/recent/ticker-posts

MWANACHAMA WA TALGWU AUAWA KINYAMA NA WAFUGAJI WILAYANI KILWA


Katibu mkuu TALGWU, Rashid M. Mtima 

***

Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU) kimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Mwanachama na kiongozi wetu Ndg. Madadi Omari Litumbui aliyekuwa Mtendaji wa Kijiji cha Mtumbei Mpopela Kata ya Kandawale Tarafa ya Kipatimu Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa. 

Hayo yamesemwa leo na Katibu Mkuu wa TALGWU Ndg. Rashid M. Mtima wakati akizungumza na waandishi wa Habari Edema hoteli mkoani Morogoro.

Mtima amesema mpaka umauti unamfika Ndg. Madadi Omari Litumbui alikuwa anahudumu katika chama cha TALGWU kama Katibu wa Kamati ya Uratibu Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa.

Mtima amesema kifo cha Mwanachama wao huyo  kilitokea tarehe 17 Machi 2024 ambapo alichomwa mkuki na Wafugaji (Wamang'ati) na aliwahishwa Kituo cha Afya Nanjilinji (Kilwa) lakini alifariki usiku huohuo wa tarehe 17/03/2024. 

Amesema tukio hilo lilitokea pindi marehemu Madadi Omar Litumbui anatekeleza majukumu yake kama Mtendaji wa Kíjiji ambapo alikuwa na wenzake katika doria ya hifadhi ya msitu wa Serikali uliounganisha Vijiji na kuwa hifadhi moja. 

Ameongeza kwa kuwa pindi Madadi na wenzake  wanawaondoa wafugaji (Wamang'ati) katika hifadhi hiyo ndipo wafugaji hao waliporusha mkuki uliomchoma Ndg. Madadi na kupelekea kifo chake.

Mtima amesema TALGWU inalaani vikali mauaji ya Mwanachama wao Madadi Omari Litumbui. 

Amesema TALGWU itafuatilia kwa ukaribu kuhakikisha haki inatendeka na ameliomba Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wale wote waliohusika na mauaji hayo ya kinyama.

Post a Comment

0 Comments