Ticker

6/recent/ticker-posts

Isanzu, Kadio watikisa fainali michuano ya gofu kumuenzi Lina

Na Mwandishi Wetu

MCHEZA gofu wa ridhaa kutoka klabu ya TPC mkoani Kilimanjaro, Ally Isanzu na mcheza gofu wa kulipwa kutoka Dar es Salaam, Hassan Kadio wameibuka vinara wa raundi ya pili ya michuano ya gofu ya Lina PG yaliyomalizika hivi karibuni mjini Morogoro.

Licha ya ushindi wao ambao unawaweka katika nafasi nzuri ya kukata tiketi ya kucheza katika michuano ya kimataifa katika Falme za Kiarabu mabingwa hao pia walizawadiwa donge nono la fedha kwa ushindi wao.

Kadio ambaye alikuwa mshindi wa kwanza katika mashindano hayo alijizolea kitita cha Sh. Milioni 6.8 huku Isanzu akiondoka na Sh. Milioni 2 kama mshindi wa gofu ya ridhaa.

Licha ya kuwa bora katka kitengo cha ridhaa, Isanzu ndiye alikuwa na matokeo bora zaidi katika michuano hiyo baada kupata mikwaju 74,73,72 na 78 katika siku nne za michuano ambazo ilipitia mashimo 72.

Isanzu alimaliza na matokeo ya jumla ya +9 na kufuatiwa na Kadio mwenye matokeo ya +12. Aidha mchezaji Abddalah Yusuf aliyepata jumla ya alama +16 alikuwa wa pili kwa wachezaji wa kulipwa mbele ya mshindi wa tatu Nuru Mollel aliyepata alama +17.

Bryszon Nyenza ambaye alimaliza na + 18 alikuwa wa nne wakati nafasi ya tano ikienda kwa Isack Wanyeche aliyerudisha alama +22

Washindi watakaokwenda Dubai ni wale wenye matokeo mazuri ya jumla baada ya kumalizika kwa raundi ya tano za mashindano hayo.

Baada ya raundi ya pili ya Morogoro, Arusha Gymkhana sasa itakuwa ni mwenyeji wa raundi ya tatu na kwa mujibu wa Mkurugenzi wa michuano hiyo, Yasmin Challi amesema kuwa raundi ya tatu itachezwa mwezi Julai mwaka huu.

Amesema kuwa wachezaji wengine katika kiwango cha kumi bora walikuwa ni Fadhil Nkya, Frank Roman, Salum Dilunga Ninja, na Athumani Chiundu.

Kwa upande wa wachezaji gofu ya ridhaa, baada ya Isanzu aliyemaliza kwa alama +9, nafasi ya pili ilichukuliwa na Isiaka Daudi Mtubwi mwenye +24 wakati Michael Massawe aliyemaliza na alama +30, alikuwa wa tatu na nafasi yha nne kushikwa na Victor Joseph mwenye alama +30 wakati nafasi ya tano ilishikwa na Seif Mcharo mwenye alama +32.

Post a Comment

0 Comments