Ticker

6/recent/ticker-posts

MWENYEKITI WA BODI TBS AFURAHISHWA UTENDAJI KAZI OFISI ZA MPAKANI

Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ikiongozwa na Mwenyekiti Profesa Othman Chande Othman imetembelea ofisi za TBS zilizopo mipaka ya Namanga, Holili, Tarakea na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).

Ziara hiyo imefanyika kuanzia tarehe 3 Juni hadi Juni 5 mwaka huu ambayo ilihusisha mipaka iliyopo kwenye mikoa ya Arusha na Kilimanjaro.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ziara hiyo, Profesa Othman Chande, alisema lengo la ziara hiyo ilikuwa ni kuona hali ya utendaji kazi wa ofisi hizo za mipakani pamoja na kujua changamoto mbalimbali ambazo wanazipitia ili ziweze kupatiwa ufumbuzi.

Profesa Othman kupitia ziara hiyo alisema wameridhishwa na utendaji wa wafanyakazi wa ofisi hizo na wamehimizwa kuendelea kufanya kazi kwa weledi ili kuwezesha biashara kufanyika kwa urahisi.

Alisema dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ni kuwezesha biashara, hivyo wafanyakazi hao wana wajibu wa kuendelea kufanyakazi kwa weledi ili kutimiza dhamira hiyo ya Rais.

Kwa mujibu wa Profesa Othman, Bodi imeridhishwa na utendaji TBS mipakani na wametaka waendelee kufanyakazi kwa bidii na kuhakikisha bidhaa zinazoingia zimekidhi matakwa ya viwango husika.

Post a Comment

0 Comments