Ticker

6/recent/ticker-posts

TBS YAWATAKA WAZALISHAJI WA BIDHAA ZA CHUMA KUZINGATIA MATAKWA YA VIWANGO


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limewataka wazalishaji wa bidhaa za Chuma aina ya Flat Bars, Square and Round Pipes kuzalisha na kuuza bidhaa zilizokidhi viwango ili kuepuka madhara ya kiafya na kiuchumi.

Wito huo umetolewa leo Juni 10,2024 na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dlt. Athuman Ngenya wakati wa Mkutano kati ya TBS na wadau hao katika Ofisi za TBS, Ubungo Jijini Dar es Salaam.

Amesema hivi karibuni wataanza kupita katika viwanda vinavyozalisha bidhaa hizo kukagua kama wanaendelea kuzalisha bidhaa zisizokidhi viwango na kuweza kuwachukulia hatua ikiwemo kuvifungia viwanda ambavyo havifuate taratibu.

Aidha amesema mojawapo ya matakwa muhimu ya viwango vya bidhaa za chuma zinazozalishwa au kuingizwa nchini ni pamoja na kuandikwa taarifa zinazoonesha jina la mzalishaji pamoja na ukubwa wa bidhaa (english name).

"Taarifa hizo ni muhimu kwa wanunuzi na watumiaji wa bidhaa kwani huwezesha kutoa mrejesho kwa mzalishaji husika pamoja na kufanya ufuatiliaji (tracebility) endapo itabainika kuwa na kasoro yoyote". Amesema Dkt. Ngenya.

Pamoja na hayo amesema uwepo wa taarifa muhimu kwenye bidhaa huziwezesha taasisi za udhibiti kuna na uwezo wa kuzitambua, kuzifanyia ufuatiliaji katika soko (market surveillance) na kuchukua hatua stahiki kwa mzalishaji atakayebainika kukiuka matakwa ya sheria, Kanuni na Viwango.

Ameeleza kuwa pamoja na jitihada zilizofanywa na TBS ili kuhakikisha bidhaa hizo zinaandikwa taarifa muhimu ikiwa ni pamoja kutoa muda maalum (grace period) ili kuhakikisha mnatekeleza takwa hilo muhimu, bado kuna baadhi ya wazalishaji ambao hawajatekeleza, na hivyo kusababisha changamoto katika udhibiti.
 
Hata hivyo amesema TBS haitasita kuchukua hatua kwa mujibu wa Sheria kwa yeyote yule atakayezalisha bidhaa za flat bars, square pipes na round pipes kinyume na matakwa ya viwango.

Kwa upande wake Ibrahimu Haji Kutoka Kampuni ya Alaf, amesema wataendelea kuzalisha bidhaa zinazokidhi viwango ili kuendana na ushindani wa biashara nchini.

Amesema kupitia kikao hicho, watayachukua maelekezo yote ambayo wamepewa na wataalamu kutoka TBS na kuyafanyia kazi ili kuendelea kuzalisha bidhaa bora na zenye viwango.

Post a Comment

0 Comments