Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba Kabudi, ameshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Jumuiya ya Madola yaliyofanyika jijini London, Uingereza, yakihusisha nchi wanachama 56 wa jumuiya hiyo.
Sherehe hiyo ilijumuisha matukio mbalimbali, ikiwemo hafla ya kupandisha bendera katika Bunge la Uingereza, uwekaji wa shada la maua katika Milango ya Kumbukumbu ya Jumuiya ya Madola, pamoja na ibada ya waumini wa dini mbalimbali iliyofanyika katika Kanisa la Westminster Abbey.
Kaulimbiu ya mwaka huu ilikuwa “Kufungua Fursa kwa Ajili ya Jumuiya ya Madola Yenye Mafanikio,” ikilenga kuhimiza diplomasia, kubadilishana tamaduni na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola.
Hafla hiyo pia iliwakutanisha wanadiplomasia, mawaziri, viongozi wa kimataifa pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo, waliotafakari kuhusu mshikamano wa muda mrefu wa Jumuiya ya Madola na umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kukuza maendeleo endelevu, huku ikichangia kuimarisha sauti na ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya kimataifa.









0 Comments