Ticker

6/recent/ticker-posts

BENKI YA NBC YAKABIDHI VIFAA TIBA KWA AJILI YA MAABARA INAYOTEMBEA ZANZIBAR




Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui (wa pili kushoto) akipokea moja ya vifaa vifaa tiba vitakavyotumika kwenye maabara inayotembea (Mobile clinic) kutoka kwa maofisa waandamizi wa benki ya NBC wakiongozwa na Mkurugenzi wa wateja binafsi wa benki hiyo Bw Elibariki Masuke (wa pili kulia)wakati wa hafla hiyo iliyofanyika ofisini kwa waziri huyo, Zanzibar. Vifaa hivyo vimetolewa benki hiyo kwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuboresha huduma ya afya hususani ya mama na mtoto visiwani humo.


Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui (alieketi) akizungumza na maofisa waandamizi wa benki ya NBC wakiongozwa na Mkurugenzi wa wateja binafsi wa benki hiyo Bw Elibariki Masuke (kushoto) wakati wa makabidhiano ya vifaa hiyo yaliyofanyika ofisini kwa waziri huyo Zanzibar. Wengine ni pamoja na Meneja wa benki ya NBC tawi la Zanzibar Bw Ramadhani Lesso (Kulia) na Mkuu wa Idara ya Huduma za Kiislam wa Benki hiyo Mohamed Nuh


Mkurugenzi wa wateja binafsi wa benki hiyo Bw Elibariki Masuke akisaini kitabu cha wageni alipoingia kwenye ofisi ya Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui wakati wa makabidhiano hayo.


Mkurugenzi wa wateja binafsi wa benki hiyo Bw Elibariki Masuke (kulia) akisalimiana na Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui wakati wa makabidhiano hayo.


Meneja wa benki ya NBC tawi la Zanzibar Bw Ramadhani Lesso (Kulia) akisalimiana na Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui wakati wa makabidhiano hayo.

Zanzibar: Agosti 27, 2021: Benki ya Taifa ya Biashara NBC, hii leo imekabidhi msaada wa vifaa tiba ikiwemo mashine ya UtraSound vitakavyotumika kwenye maabara inayotembea (Mobile clinic) ambayo pia imetolewa na benki hiyo kwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuboresha huduma ya afya hususani ya mama na mtoto visiwani humo.

Akizungumza mara baada ya kupokea vifaa hiyo vyenye thamani ya zaidi ya Sh mil 19.5 Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui pamoja na kuishukuru benki hiyo kwa msaada huo, alisema serikali hiyo itahakikisha msaada huo utatumika kama ilivyokusudiwa.

“Msaada huu ni muhimu na kiukweli unahitajika sana. Jukumu letu kama serikali ni kuhakikisha vifaa hivi vinatunzwa na vinatumika kama ilivyokusudiwa ili vilete tija iliyolengwa kwa maana visaidie haswa kuokoa maisha ya wazanzibar wakiwemo wakina mama na watoto hasa walipo pembezoni.

Aliahidi kwa niaba ya serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuendeleza ushirikiano na benki hiyo hususani kwenye masuala mbalimbali ikiwemo yale yanayohusu ustawi wa jamii huku akibainisha kuwa uimara wa benki hiyo kwenye utoaji wa huduma zake visiwani humo kwa kiasi kikubwa unachagizwa na namna inavyoshirikiana na jamii ya Wazanzibar ikiwemo kibiashara na mambo ya kijamii.

“Naamini kabisa uimara wa benki ya NBC tangu ilipoanza kutoa huduma zake hapa Zanzibar ni matokeo ya ushirikiano iliyonayo na jamii ya Wazanzibar…nawapongeza sana na ninaomba muendelee kuguswa zaidi,’’ aliongezea.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa wateja binafsi wa benki ya NBC Bw Elibariki Masuke alisema pamoja na msaada huo benki hiyo itaendelea kuhudumia vifaa hivyo hata pale vitakapokuwa vinapata hitirafu za kiufundi.

“Benki ya NBC tumekuwa tukiguswa na changamoto mbalimbali zilizopo kwenye huduma za afya hapa nchini ikiwemo Zanzibar na ndio maana tumekuwa mstari wa mbele kuhakikisha tunashirikiana na serikali zote mbili kukabiliana na changamoto zinazohusu sekta hii muhimu.’’

“Tunaamini kupitia vifaa hivi vitakavyofungwa ndani ya maabara inayojongea wataalamu wa afya wataweza kuwafikia walengwa popote walipo hususani wale waliopo pembezoni wakiwemo wakina mama na watoto na kupitia msaada wa Mungu tutaweza kuokoa maisha yao,’’ aliongeza.

Akizungumzia msaada huo Mratibu wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Mtoto, Wizara ya Afya Zanzibar Bi Wanu Bakari alisema msaada huo umefika wakati muafaka wakati serikali hiyo ikipambana kusogeza huduma za afya hususani maeneo ya pembezoni ili kuepukana na changamoto ya vifo vya akina mama na watoto wakati wa kujifungua.

“Tunaishukuru sana benki ya NBC kwa kuliona hili na kwa kweli wametugusa sana! Kwa mfano kupitia maabara hii tutaweza kutoa huduma ya Utrasound ambapo kwa kwasasa tunakabiliwa na uhaba wa huduma hii hivyo tatizo linakwenda kupungua. Zaidi pia miongoni mwa vifaa hivi pia vipo vifaa vya uchunguzi wa afya za kina mama wajawazito kitu ambacho kitatusaidia kuwafanyia uchunguzi kwa haraa pale itakapohitajika kabla hawajapata madhara zaidi,’’ aliongezea.

Post a Comment

0 Comments