Ticker

6/recent/ticker-posts

DC KISWAGA : TAMASHA LA MICHEZO, AFYA NA MAONESHO YA BIASHARA KAHAMA KUANZIA AGOSTI 23,2021



Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga
Na Salvatory Ntandu - Kahama


Zaidi ya wafanyabiashara 3000 kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania wanatarajia kushiriki mazoezi ya viungo ili kujikinga na ugonjwa wa Uviko 19 pamoja na Maonesho ya Biashara yatakayofanyika katika uwanja wa taifa wilayani Kahama mkoani Shinyanga kuanzia Jumatatu Agosti 23 hadi Agosti 29,2021.


Kauli hiyo imetolewa leo Jumapili Agosti 22,2021 na Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Tamasha la Michezo, Afya na Biashara litakalohusisha mazoezi sambamba na maonesho ya biashara likalofanyika wilayani humo kuanziaAgosti 23 hadi 29 mwaka huu.


Amesema serikali kwa kushirikiana nakituo cha uwezeshaji wananchi kiuchumi kahama wameaandaa mazoezi hayo ya siku saba yatakayokwenda sambamba na maonesho ya biashara ili kutoa fursa kwa wananchi wa Kahama kutangaza bidhaa wanazozizalisha.


"Tunahamasisha wananchi na wafanyabiashara kufanya mazoezi ili kujikinga na ugonjwa wa Corona lakini pia waendelee na kazi za uzalishaji mali au biashara ili kukuza vipato vyao," alisema Kiswaga.


Kiswaga amefafanua kuwa mazoezi hayo yanalenga kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassani katika mapambano dhidi ya gonjwa la Corona kwa kuwahimiza wananchi kutenga muda wa kufanya mazoezi ili kuimarisha afya zao.


"Kauli mbiu yetu ya mazoezi haya inasema fanya mazoezi ujikinge na Uviko - 19 ,kazi iendelee ikiwa na dhima la kuleta hamasa kwa wananchi,wafanyabiashara,wajasiriamali kushiriki katika mazoezi hayo ambayo ni muhimu kwa afya zao,"alisema Kiswaga.


Sambamba na hilo Kiswaga amewahakikishia usalama wafanyabiashara wote watakaoshiriki mazoezi na maonesho hayo ya biashara kwa siku hizo saba.


"Tutatahakikisha huduma zote muhimu zinapatika hapa, nitoe fursa kwa wafanyabiashara wa kutoka mikoa mbalimbali kuja kutangaza biashara zao kupitia fursa hii adhimu,maafisa kutoka ofisini kwangu watakuwepo kusikiliza kero za wananchi,"alisema Kiswaga.


Kwa upande wake, Mratibu wa Tamasha la Michezo, Afya na Biashara kutoka Taasisi ya GS1 Tanzania Shabani Mikongoti amesema kuwa maandalizi yote ya mazoezi na maonesho hayo yamekamilika na kuwataka wafanyabiashara kujitokeza kushiriki maonesho hayo maalumu.


"Mpaka sasa Tent zote zimeshafungwa kuzunguka uwanja huu, tumetenga maeneo ya wafanyabiashara wakubwa na wadogo ili kutoa fursa kutangaza biashara zao kwa kipindi cha siku saba hivyo ni vyema wakajitokeza mapema kutumia fursa hiyo adhimu,"amesema Mikongoti.

Post a Comment

0 Comments