Ticker

6/recent/ticker-posts

RAIS SAMIA AMEDHAMIRIA KUMSHUSHA MAMA NDOO KICHWANI - MAJALIWA


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Kiwanda cha Maji cha Swahili cha Nangurukuru wilayani Kilwa, Hosseah Hopaje wakati alipotembelea kiwanda hicho, Oktoba 6, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama maji yaliyowekwa kwenye chupa wakati alipotembelea kiwanda cha Swahili cha Nangurukuru wilayani Kilwa, Oktoba 6, 2021. Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda hicho, Hosseah Hopaje. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama chupa kubwa za maji wakati alipotembelea kiwanda cha maji cha Swahili katika eneo la Nangurukuru wilayani Kilwa, Oktoba 6, 2021. Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda, Hosseah Hopaje. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kuhusu kiwanda cha maji cha Swahili cha Nangurukuru wilayani Kilwa kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda, Hosseah Hopaje wakati alipotembelea kiwanda hicho, Oktoba 6, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

*****************************

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Meneja wa RUWASA Wilaya ya Kilwa, kufanya utafiti wa kina wa maeneo ambayo yatawezesha upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo yote yenye changamoto ya maji katika wilaya hiyo.



Amesema Serikali inayoongozwa na mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuhakikisha huduma ya maji safi na salama inapatikana katika kila kijiji ikiwa ni utekelezaji wa kampeni yake ya kumtua mama ndoo kichwani.



Ametoa maagizo hayo leo (Jumatano Oktoba 6, 2021) wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na wakazi wa vijiji vya Nasaya, Chumo na Kipatimu akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Lindi.



“Utafiti lazima ufanyike ili tujue wapi tunapa maji, Rais Samia anatoa pesa kwa ajili ya kuwahudumia wananchi, piteni mpime maeneo yote mtafute vyanzo na mtuambie maji yako kiasi gani, mitambo na wataalam tunao.”



Awali, akizungumza na wananchi wa kijiji cha Chumo, Waziri Mkuu ametoa onyo kwa wafugaji wenye tabia ya kuingiza mifugo katika mashamba ya wakulima. “Viongozi wekeni utaratibu wa kukutana na wafugaji na kuwaelimisha ili wafuge kulingana na ukubwa wa maeneo yao.”



Waziri Mkuu amesema kuwa Serikali inaendelea na mpango wake wa kuunganisha mtandao wa barabara Wilaya kwa Wilaya baada ya kukamilika kwa mpango wa kuunganisha makao makuu ya mikoa kwa barabara za lami.



“Meneja wa TANROADS nimeona ukarabati unaoendelea hakikisha barabara hii inafanyiwa ukarabati wa mara kwa mara na iwe inapitika kipindi chote.”



Akiwa katika kijiji cha Miteja Waziri Mkuu alimuagiza Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, Zainab Kawawa asimamia ujenzi wa Kituo Shikizi cha Masaninga ambacho kimejengwa kwa nguvu ya wananchi hadi kufikia hatua ya upauaji.

Amesema hadi kufikia tarehe 4 ya mwezi Novemba shule hiyo iwe imekamilika na kuchangia shilingi milioni tano ikiwa ni hatua ya kuunga mkono jitihada za wananchi wa kijiji hicho.



Katika hatua nyingine Waziri Mkuu alitembelea kiwanda cha kusindika vinywaji cha Hopaje kilichopo Nangurukuru Wilayani Kilwa, ambapo amesema Mheshimiwa Rais Samia ameendelea na utekelezaji wa sera ya viwanda na kuvutia wawekezaji ili kukuza uchumi kwa kuweka mazingira bora ya uwekezaji.

Post a Comment

0 Comments