Ticker

6/recent/ticker-posts

WAFUGAJI WATAKIWA KUMILIKI MAENEO KIHALALI NA KUYATUNZA


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na wananchi wa vijiji vya Kapele na Ikana ambapo amewataka wananchi hao kuheshimiana kulingana na kazi wanazofanya kwani kwa kufanya hivyo kutasaidia kuondoa migogoro iliyopo ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.


Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Nyanda za Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo, Dkt. Asimwe Rwiguza akiwahamasisha wananchi (wafugaji) wa Kijiji cha Kapele kuhakikisha wanakuwa na mashamba ya malisho ya mifugo yao lakini pia Halmashauri za Wilaya Nchini kutenga maeneo kwa ajili kilimo cha malisho ili wafugaji waanze kujifunza na kuanza kulima malisho katika maeneo yao.

.........................................................................

Wafugaji hapa nchini wametakiwa kumiliki maeneo kwa kutumia njia halali na kuhakikisha wanayaendeleza ikiwa ni pamoja na upandaji wa malisho katika maeneo hayo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki wakati alipofanya mikutano na wananchi wa vijiji vya Kapele, Ikana, Mpapa na Samang’ombe wilayani Momba mkoani Songwe alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi.

Waziri Ndaki amesema wafugaji wanatakiwa kutambua kuwa wanatakiwa kumiliki maeneo kihalali kwa ajili ya kufanyika shughuli za ufugaji kama ambavyo wakulima na watumiaji wengine wa ardhi wanavyomiliki.

"Wafugaji mnatakiwa kumiliki maeneo kihalali ambayo ukubwa wake utaendana na idadi ya mifugo mnayotaka kufunga na kuhakikisha mnayatunza na kuyaendeleza," alisema Waziri Ndaki

Pia Waziri Ndaki amesema Halmashauri zote nchini zinatakiwa kutenga maeneo kwa ajili ya wafugaji na malisho ya Mifugo ambayo yatalindwa kisheria na kukabidhiwa kwa wafugaji. Yapo maeneo ambayo yametengwa katika vijiji kwa ajili ya shughuli za ufugaji lakini bado hayajakabidhiwa kwa wafugaji.

Aidha, wafugaji wameshauriwa kuanza kuvuna mifugo yao pale wanapoona idadi ya mifugo imekuwa kubwa kuliko eneo wanalolimiliki. Hivyo amewasihi kuanza kuvuna mifugo ili wabaki na mifugo inayoendana na ukubwa wa maeneo wanayoyamiliki.

Vilevile amesema kuwa moja ya sababu ya migogoro ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi hasa wakulima ni suala la malisho. Hivyo amewataka wafugaji kuanza kupanda malisho katika maeneo watakayoyamiliki na kuacha kutegemea malisho ya asili peke yake.

Kuhusu malalamiko ya wakulima kupigwa na wafugaji, Waziri Ndaki amewataka wafugaji na wakulima kuheshimiana kila mmoja kulingana na shughuli wanazofanya kwani kwa kufanya hivyo hakutakuwa na migogoro. Lakini pia ameuagiza uongozi wa wilaya uhakikisha wanawachukulia hatua za kisheria wafugaji ambao watabainika kuwa wamewapiga wakulima.

Post a Comment

0 Comments