Ticker

6/recent/ticker-posts

MIGODI ILIYOANZISHWA KABLA YA SHERIA YA MAZINGIRA YA MWAKA 2004 INACHANGAMOTO NYINGI-DKT.GWAMAKA

Wataalamu wa mazingira kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na utunzaji wa mazingira (NEMC) wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Samuel Gwamaka wakitembelea mradi wa mgodi tarajiwa wa Nyanzaga uliopo Kata ya Igalula Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza unaomilikiwa na Kampuni ya SOTTA MINING CORPORATION. Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Samuel Gwamaka wa sita kutoka kulia akiwa katika picha ya pamoja na wamiliki wa mgodi tarajiwa wa uchimbaji wa dhahabu wa Nyanzaga pamoja na Wataalamu kutoka NEMC alipotembelea mgodi huo tarajiwa uliopo Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza. Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) wa tatu kutoka kushoto akipata maelezo kutoka kwa Afisa Mazingira wa kampuni ya SOTTA inayotarajia kuanza kuchimba dhahabu Bw. Delphine Kaballega. Dkt. Gwamaka alifanya ziara kukagua na kutoa elimu kuhusu uhifadhi na utunzaji wa mazingira kabla na baada ya kuanza uchimbaji wa dhahabu.

Wataalamu wa mazingira kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na utunzaji wa mazingira (NEMC) wakisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Mazingira wa kampuni ya SOTTA Bw. Delphine Kaballega walipofanya ziara kwenye mgodi tarajiwa wa Nyanzaga Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza. Wataalamu wa mazingira kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na utunzaji wa mazingira (NEMC) wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Samuel Gwamaka wakiwa katika kikao na baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ya SOTTA inayotarajia kuanza kuchimba dhahabu Nyanzaga Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza.

***************************

Kuna ulazima kufanya tathimini ya athari kwa mazingira (TAM) na kuweka mpango mkakati wa utunzaji wa mazingira pale mgodi unapochimbwa na mwisho unapofungwa.

Ameyasema hayo leo Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira Dkt. Samuel Gwamaka alipofanya ziara kwenye mradi wa mgodi tarajiwa wa Nyanzaga uliopo Kata ya Igalula Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza unaomilikiwa na Kampuni ya SOTTA MINING CORPORATION.

"Mgodi unapoanzishwa ni lazima ufanyiwe Tathmini ya Athari ya Mazingira na mpango mkakati wa utunzaji wa mazingira kabla kuanzishwa, unapochimbwa na hatimaye unapofunga ili kulinda mazingira yetu." Dkt. Gwamaka.

Dkt. Gwamaka amesema kuwa migodi iliyoanzishwa kabla ya Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 inachangamoto nyingi ikiwa ni pamoja na migogoro ya kimazingira kati yake na jamii, pamoja na Serikali kuingia gharama kubwa ya kurekebisha mazingira yaliyoharibika.

"Hasara nyingine ya kutokuweka mpango mkakati wa namna ya ufungaji wa migodi pindi unapofungwa ni pamoja na kuacha mazingira katika hatari kwa afya ya jamii na viumbe wengine hai." Dkt. Gwamaka.

Ni mkakati wa Baraza kuhakikisha historia mbaya ya utunzaji wa mazingira kwa migodi iliyoanzishwa kabla ya Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 hayatajitokeza tena kwenye migodi itakayoanza kuchimbwa kwenye awamu hii ya Sita ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Naye Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria kutoka NEMC Mhandisi Redempta Samwel amepongeza hatua zinazochukuliwa na mradi wa uchimbaji wa madini ya dhahabu wa Nyanzaga katika kuhakikisha mazingira yanatunzwa kuanzia hatua ya awali kabla ya shughuli za uchimbaji kuanza.

Pia, Mhandisi Redempta ameongeza kuwa Baraza lina wajibu na mamlaka ya Kisheria ya kufuatilia utekelezaji wa mpango mkakati ili kuepusha athari za kimazingira zinazoweza kujitokeza.

Wakati huo huo Meneja wa Kanda ya Ziwa Viktoria NEMC Jerome Kayombo amesema mgodi tarajiwa wa Nyanzaga utakuwa ni wa mfano kwa migodi mingine kwasababu umeanza ushirikiano na sisi wataalamu wa mazingira kuanzia hatua za mwanzo kabisa, hii itasaidia kuweka mipango mikakati ya kuzuia uharibifu wa mazingira.

"Sisi Baraza tunahakikisha anayeanzisha mgodi amefanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) pamoja na kuweka mpango mkakati wa utunzaji wa mazingira." Bw. Kayombo.

Nao uongozi wa mgodi tarajiwa umepongeza sana NEMC kuwa Taasisi ya Kwanza kufika mgodini hapo mara baada ya kupata cheti cha mazingira na wameahidi kushirikiana nao bega kwa bega kuhakikisha mazingira yanalindwa kwa ajili ya maendeleo endelevu.

Post a Comment

0 Comments