Ticker

6/recent/ticker-posts

RIDHIWANI KIKWETE AAGIZA WATENDAJI ARDHI KUWEKEWA VIPIMO VYA UTENDAJI KAZI


Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na watumishi wa sekta ya ardhi katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani wakati wa ziara yake katika mkoa wa Dar es Salaam tarehe 8 Januari 2022.

Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dar es Salaam Idrisa Kayera akizungumza katika kikao baina ya Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Ridhiwani Kikwete na watumishi wa sekta ya ardhi wakati wa ziara yake katika mkoa wa Dar es Salaam tarehe 8 Januari 2022.

Sehemu ya watumishi wa sekta ya ardhi wakimsikiliza Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Ridhiwani Kikwete (Hayupo pichani) wakati wa ziara yake katika mkoa wa Dar es Salaam tarehe 8 Januari 2022. Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Ridhiwani Kikwete akimuangalia mtoto aliyemkuta Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati wa ziara yake katika mkoa huo tarehe 8 Januari 2022.

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Ridhiwani Kikwete akiongozwa na Katibu Tawala mkoa wa Dar es Salaam Hassan Abbas Rugwa alipofika katika ofisi ya mkuu wa mkoa wakati wa ziara yake katika mkoa huo tarehe 8 Januari 2022.

******************************

Na Munir Shemweta, WANMM

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Ridhiwani Kikwete amewaagiza Makamishna wa Ardhi Wasaidizi wa mikoa nchini kuhakikisha wanawawekea vipimo vya utendaji kazi watumishi wa sekta ya ardhi kila baada ya mwezi mmoja ili kupima utendaji wao kwa lengo la kuleta tija kwenye sekta ya ardhi.

Aidha, aliwataka wataalamu wa sekta ya ardhi nchini kuwa, wabunifu sambamba na kutoa huduma bora na kwa wakati ili kuisaidia serikali na wananchi kwa ujumla.

Ridhiwani alitoa agizo hilo leo tarehe 8 Januari 2022 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na watendaji wa sekta ya ardhi wa mkoa huo na baadhi ya watumishi wa sekta hiyo katika mkoa wa Pwani akiwa kwenye ziara yake katika mkoa huo kufuatia kuteuliwa kushika nafasi hiyo hivi karibuni.

‘’Makamishna wangu, haya sasa ni maagizo, hao maafisa wenu wote, katika idara zenu zote wawekeeni vipimo vya kupima utendaji kila baada ya mwezi mmoja ili kujua nani anafanya kazi na nani hafanyi kazi. Kujua idara gani inafanya kazi na idara gani haifanyi kazi’’ alisema Ridhiwani.

Alisema, kama watendaji wa sekta ya ardhi wataendelea kufanya kazi kwa mazoea na kuzalisha migogoro kila siku basi sekta ya ardhi haitapiga hatua. Alieleza kuwa, baaadhi ya watendaji wa sekta ya ardhi nchini ni mafundi wa kuzalisha migogoro na baadaye hupita mlango wa nyuma kujifanya wanakwenda kuimaliza jambo alilolieleza kuwa, Wizara yake haiko tayari kuvumilia tabia hiyo kwa kuwa upo Mfumo Unganishi wa Taarifa za Ardhi (ILMIS) unaoweza kuzitafutia ufumbuzi baadhi ya changamoto za ardhi.

‘’Mfumo wetu wa ILMIS uko vizuri na umeanza mkoa wa Dar es Salamaa na tunataka kuupeleka mikoa mikubwa na baadaye nchi nzima maana tufikie mahalali majawabu ya shida zetu tuweze kuyapata kupitia mfumo.

Aidha, Naibu Waziri wa Ardhi alisema, hatakuwa tayari kusikia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anabebeshwa lawama asizostahili kuhusiana sekta ya ardhi kuweka bayana kuwa, kama yupo mtu anayedhani anaweza kufanya jambo la hovyo basi ajue utaratibu huo umekwisha.

Aliwataka wataalamu wa sekta ya ardhi kuwa wabunifu sambamba na kutoa huduma bora na kwa wakati na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kuisaidia serikali na wananchi kwa ujumla.

‘’Nawaomba muwe wabunifu na muache kufanya business as usual kama kazi yako ni afisa ardhi usipoletewa vifaa eti unalala, hiyo haiwezekanni na kama hakuna vifaa waombe wakubwa zako ili wao waone sababu ya kupeleka vifaa ili upime ardhi kwa kuwa ardhi ni uchumi’’. Alisema Ridhiwani.

Post a Comment

0 Comments