Ticker

6/recent/ticker-posts

MKUTANO WA 15 WA BARAZA LA MAWAZIRI LA KISEKTA LA NISHATI LA EAC WAFUNGULIWA JIJINI ARUSHA KATIKA NGAZI YA WATAALAMU

Mkutano wa 15 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki umefunguliwa leo tarehe 8 Februari 2022 jijini Arusha, Tanzania katika ngazi ya Wataalamu.

Mkutano huu utafanyika katika ngazi tatu ambapo umeanza na; Mkutano Ngazi ya Wataalamu unaofanyika tarehe 8 hadi 9 Februari 2022, utafuatiwa na Mkutano Ngazi wa Makatibu Wakuu utakaofanyika tarehe 10 Februari 2022 na utamalizika kwa Mkutano Ngazi ya Mawaziri utaofanyika tarehe 11 Februari 2022.

Lengo la Mkutano huu ni kupitia na kuandaa taarifa ya hali ya utekelezaji wa Maamuzi/Maagizo ya mikutano iliyopita; Hatua iliyofikiwa hadi sasa katika sekta za Nishati Umeme, Nishati Mafuta, na Nishati Jadidifu; pamoja na Utekelezaji wa Miradi/Programu mbalimbali za Kitaifa na Kikanda ya Sekta za Nishati inayotekelezwa ndani ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki.

Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano Ngazi ya Wataalamu unaongozwa na Kamishna Msaidizi Maendeleo ya Umeme kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Styden Rwebangila ambaye ameambatana na Mkurugenzi Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Eliabi Chodota, Mkurugenzi Idara ya Nishati na Madini kutoka Wizara ya Nishati na Madini Zanzibar, Mhandisi Said H. Mdungi pamoja na maafisa wengine Waandamizi kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wenye dhamana katika sekta ya nishati.

Mkutano Ngazi ya Wataalamu na Ngazi ya Makatibu Wakuu ni sehemu ya mikutano ya awali kwaajili ya maandalizi ya Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki utaofanyika tarehe 11 Februari 2022.
Kushoto ni Kiongozi wa ujumbe wa Tanzania katika Mkutano Ngazi ya Wataalamu na Kamishna Msaidizi wa Maendeleo ya Umeme katika Wizara ya Nishati, Mhandisi Styden Rwebangila na kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Eliabi Chodota akifafanua jambo wakati wa majadiliano ya mkutano huo.
Mwenyekiti wa Mkutano Ngazi ya Wataalamu na Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu kutoka Jamhuri ya Kenya, Mhandisi Benson Mwakina (Kushoto) akiongoza majadiliano, kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia Sekta za Uzalishaji na Jamii, Bw. Christophe Bazivamo.
Kushoto ni Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhandisi Mgeta Sabe na wajumbe wengine wa Tanzania wakifatilia majadiliano.
Mkutano ukiendelea
Ujumbe wa Tanzania.
Sehemu nyingine ya Ujumbe wa Tanzania.


Post a Comment

0 Comments