Ticker

6/recent/ticker-posts

MAKAMU WA RAIS DKT.MPANGO AMUWAKILISHA RAIS KATIKA IBADA YA SHEREHE YA JUBILEI YA DHAHABU YA MIAKA 50


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango akisalimiana na Mhashamu Askofu Method Kilaini ambaye ni Askofu Msaidizi Jimbo Katoliki la Bukoba kabla ya kuanza kwa Ibada ya shukrani ya Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya Upadre wa Mhashamu Askofu Method Kilaini leo tarehe 19 Machi 2022 Bukoba Kagera.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango akishiriki Ibada ya shukrani ya Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya Upadre wa Mhashamu Askofu Method Kilaini iliofanyika Kanisa Kuu Katoliki wilayani Bukoba mkoani Kagera leo tarehe 19 Machi 2022.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango akizungumza na viongozi wa dini, waumini na viongozi wa serikali mara baada ya Ibada ya shukrani ya Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya Upadre wa Mhashamu Askofu Method Kilaini iliofanyika Kanisa Kuu Katoliki wilayani Bukoba mkoani Kagera leo tarehe 19 Machi 2022.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango na mkewe Mama Mbonimpaye Mpango wakimkabidhi zawadi Mhashamu Askofu Method Kilaini mara baada ya kushiriki Ibada ya shukrani ya Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya Upadre wa Askofu Kilaini iliofanyika Kanisa Kuu Katoliki wilayani Bukoba mkoani Kagera leo tarehe 19 Machi 2022.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango akiagana na Mhashamu Askofu Method Kilaini ambaye ni Askofu Msaidizi Jimbo Katoliki la Bukoba mara baada ya Ibada ya shukrani ya Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya Upadre wa Mhashamu Askofu Method Kilaini leo tarehe 19 Machi 2022 Bukoba Kagera.

**********************

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango leo tarehe 19 Machi 2022 amemwakilisha Rais Samia Suluhu Hassa katika Ibada na sherehe ya Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya Upadre wa Mhashamu Askofu Method Kilaini ambaye ni Askofu Msaidizi Jimbo Katoliki la Bukoba. Ibada hiyo imefanyika katika kanisa kuu katoliki wilayani Bukoba mkoani Kagera.

Akizungumza mara baada ya ibada hiyo, Makamu wa Rais amesema Serikali inatambua na kushukuru kwa mchango wa Baba Askofu Kilaini katika Kanisa na pia kwa jamii ya Watanzania. Amemtaja Askofu Kilaini kama miongoni mwa waanzilishi wa Kamati ya Amani ya Viongozi wa Dini (1994) ambayo imeimarisha maelewano miongoni mwa waumini wa dini na madhehebu mbalimbali hapa nchini.



Aidha amelipongeza na kulishukuru Kanisa Katoliki kwa kuunga mkono juhudi za Serikali na kwa kutoa mchango mkubwa katika ustawi wa Taifa kiroho, kiuchumi na kijamii. Amesema Kanisa limeweza kufikisha huduma za kijamii katika maeneo mbalimbali nchini, yakiwemo yale ambayo Serikali bado haijaweza kufikisha huduma hususani vijijini na maeneo wanakoishi watu wa hali ya chini mijini. Aidha amelipongeza kanisa kwa kuendelea kuhudumia yatima na watoto wanaoishi katika mazingira magumu.



Makamu wa Rais amesema serikali imejielekeza katika kuboresha na kujenga miundombinu ya usafiri na usafirishaji, miundombinu ya Elimu, afya na maji katika mkoa wa Kagera ili kuweka mazingira mazuri ya kuvutia wawekezaji wa ndani na nje, kwenye viwanda vya kuchakata mazao ya kilimo na uchimbaji wa madini kama mgodi wa Nikel Kabanga na kufungua fursa za biashara na ajira hivyo kuwaasa wananchi wa Kagera kutumia fursa hizo kukuza uchumi wao.



Halikadhalika Dkt. Mpango ameliasa kanisa kufundisha na kulea vijana katika maadili mema na kuthamini kufanya kazi halali. Amesema katika nyakati hizi, kuna ongezeko la mmomonyoko mkubwa wa maadili katika jamii ikiwemo ulevi, vitendo vya rushwa, uvivu, wizi na ufisadi, mauaji ya kutisha na idadi kubwa ya ndoa kuvunjika na kuongezeka kwa watoto wa mitaani.



Pia Makamu wa Rais amewaasa viongozi wa Kanisa Katoliki na madhehebu mengine yote ya dini kupaza sauti kuhamasisha usafi, ulinzi na uhifadhi wa mazingira.



Kwa upande wake Askofu Method Kilaini ameishukuru serikali kwa ushirikiano iliyompatia kwa kipindi chote cha miaka hamsini ya utumishi wake. Aidha amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa mwaka mmoja wa uongozi wake wenye mafanikio makubwa na kazi nzuri alioifanya. Amesema katika kipindi cha mwaka mmoja wa uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan taifa limeongozwa kwa utu, Amani na mshikamano pamoja na hatua mbalimbali za maendeleo kwa wananchi.



Halikadhalika Askofu Kilaini amewashukuru wananchi wa mkoa wa Kagera kwa kuwa pamoja naye wakati wote wa utumishi wake na kuwaomba kuimarisha umoja, mshikamano , Amani pamoja na kufanya kazi kwa bidii ili kuuletea maendeleo mkoa wa Kagera.

Post a Comment

0 Comments