







(PICHA ZOTE NA EMMANUEL MBATILO)
********************
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM
Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kimeandaa warsha maalumu kwaajili ya kuwajengea uwezo wanawake kukabiliana na changamoto wanazokumbana nazo kazini, nyumbani, na katika jamii.
Akizungumza katika ufunguzi wa warsha hiyo, Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji Prof.Zacharia Mganilwa amesema majukumu ya mwanamke yanaanzia nyumbani, kazini hadi kwenye jamii nzima inayomzunguka hivyo wanawake wanatakiwa kuamka na kutumia fursa zilizopo nchini kuhakikisha wanaweza kufanya mambo makubwa na kuweza kuinua uchumi wa nchi.
Amesema kuwa wanawake wakiwa mstari wa mbele kwenye masomo ya sayansi jamii itapata maendeleo haraka kwa kuwa mfumo wa maisha wa jamii wanawake wamekuwa na majukumu mengi.
Aidha Prof.Mganilwa amesema kuwa Chuo hicho wiki mbili zilizopita kimetoa timu maalumu ya hamasa iliyokwenda Mikoa ya Kusini (Lindi na Mtwara)kwenye shule za mikoa hiyo kuhamasisha wanafunzi wa kike kusoma Sayansi.
“Tunaye mwanafunzi wa kike hapa aliyepata daraja la juu la kwanza la Hesabu ambaye tukimpatia ajira hapa anapokwenda kuhamasisha wanafunzi wengine wanaona mfano nzuri, na watahamisika kuona kuwa mtaalamu wa Sayansi ni Mwanamke” amesema Prof. Mganilwa.
Ameeleza kuwa chuo hicho kina mifano mingi yenye kutoa hamasa kwa wanafunzi wa kike kusoma sayansi mathalan Mkuu wa Idara ya Komputer na Mkuu Idara ya Hesabati na Sayansi ya jamii ni wanawake .
Kwa upande wake Naibu Mkuu Fedha Mipango na Utawala wa chuo cha NIT Dkt.Zainab Mshani amesema kuwa chuo hicho kimefanya Semina kwa ajili ya wanawake kuelekea maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani.
Dkt. Mshani amesema kuwa kwenye Semina hiyo kutawasiliswa mada mbalimbali ikiwemo matatizo ya afya ya akili, na masuala ya kiuchumi.
0 Comments