Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI KUZINDUA KAMPENI YA CHANJO YA UGONJWA WA POLIO KWA WATOTO CHINI YA UMRI WA MIAKA MITANO MEI 18 HADI 21, 2022 NCHI NZIMA


Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Afya, Bi. Catherine Sungura akizungumza leo Jijini Dar es Salaam wakati wa Semina ya waandishi na wahariri wa vyombo vya habari kusuhu kampeni ya chanjo ya Polio ya matone itakayoanza kutolewa kuanzia tarehe 18 hadi 21 Mei, 2022.


Afisa Programu mpango wa Taifa wa chanjo kutoka Wizara ya Afya, Bi. Lotalis Gadau akitoa mada kwa Wahariri na waandishi wa habari katika Semina hiyo iliyofanyika leo mei 11,2022 katika ukumbi wa Anautoglou Jijini Dar es Salaam.


Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Afya, Bi. Catherine Sungura(wa pili kushoto) akiwa na wadau mbalimbali pamoja na watumishi wa Wizara hiyo wakifuatilia mada iliyokuwa ikitolewa na Afisa Programu mpango wa Taifa wa chanjo kutoka Wizara ya Afya, Bi. Lotalis Gadau (hayumo pichani) wakati wa semina hiyo Jijini Dar es salaam.


Picha mbalimbali za waandishi na waariri wa vyombo vya habari wakiwa kwenye semina hiyo.PICHA NA: HUGHES DUGILO






Na: Hughes Dugilo, DAR ES SALAAM.


Wizara ya Afya imesema kuwa imejipanga kuhakikisha watoto wote wenye umri chini ya miaka mitano wanapata chanjo ya ugonjwa wa Polio inayotarajia kuanzi kutolewa tarehe 18 hadi 21 Mei,2022.

Afisa Programu Mpango wa Taifa wa chanjo kutoka Wizara ya afya Lotalis Gadau ameyasema hayo wakati wa semina ya waandishi na wahariri wa vyombo vya habari iliyofanyika leo Mei 11,2022 Jijini Dar es Salaam iliyolenga kutoa uelewa kwa wadau hao kuhusu kampeni hiyo.

Gadau ameeleza kuwa katika kipindi cha hivi karibuni nchi ya Malawi (Lilongwe) ilitoa taarifa ya mgonjwa wa Polio na kwamba kutokana na mwingiliano wa wananchi wa Tanzania na Malawi ipo hatari ya Tanzania kupata maambukizi ya ugonjwa huo endapo hatua madhubuti hazitachukuliwa.

"Wizara ina malengo na mipango ya kuhakikisha chanjo hii inamfikia kila mtoto hapa nchini kwa usawa, tuna timu ya kutosha ambayo itasambaa mitaani hivyo tumepanga kuwafuata watoto majumbani ili kuhakikisha watoto wote wanafikiwa" amesema Gadau.


Awali akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina hiyo Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Afya, Bi. Catherine Sungura amesema kuwa lengo la kutoa semina hiyo kwa wahariri na waandishi wa habari ni kupeana uelewa kuhusu ugonjwa huo ili kuielimisha jamii kwa kutoa elimu sahihi kuhusu chanjo hiyo.

"Sio kitu kigeni kuona watoto wanapata Chanjo, na chanjo hii ni salama hivyo kampeni hii ni ya nchi nzima na tutapita nyumba kwa nyumba kuhamasisha wananchi" amesema Catherine.

Kampeni hiyo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Mei 18,2022 Jijini Dodoma ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Afya Ummy Mwalimu.

Post a Comment

0 Comments