Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI YAANDA MIONGOZO ITAKAYOSAIDIA UTEKELEZAJI WA UIMARISHAJI BORA WA ELIMU YA SEKONDARI KWA NJIA MBADALA

Katibu Tawala Mkoa wa Dar es Salaam, Rehema Madenge akitembelea mabanda ya wadau wa elimu leo Oktoba 19,2022 katika Kongamano la Maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima, katika Chuo Kikuu cha Elimu Dar es Salam (DUCE).Katibu Tawala Mkoa wa Dar es Salaam, Rehema Madenge akizungumza katika Kongamano la Maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima, yaliyofanyika leo Oktoba 19,2022 katika Chuo Kikuu cha Elimu Dar es Salam (DUCE). Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima, akizungumza katika Kongamano la Maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima, yaliyofanyika leo Oktoba 19,2022 katika Chuo Kikuu cha Elimu Dar es Salam (DUCE).

*******************

SERIKALI kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeandaa miongozo mitano ambayo inasaidia katika utekelezaji wa kuimarisha ubora wa utolewaji wa elimu ya sekondari kwa njia mbadala (SEQUIP).

Mpango huo unatambua kisomo kama haki ya msingi kwa maendeleo ya mtu binafsi, kijamii, kiuchumi na kisiasa.

Ameyasema hayo leo Oktoba 19,2022 Jijini Dar es Salaam Kaimu Kamishna wa Elimu nchini, Mwalimu Venancy Manori katika Kongamano la Maadhimisho ya Juma la Elimu ya Watu Wazima, katika Chuo Kikuu cha Elimu Dar es Salam (DUCE).

Amesema katika kipindi cha mwaka 2021, jumla ya wasichana 3,333 walijiunga na programu hiyo katika vituo 131 nchi nzima.

“Haya ni baadhi ya mambo yaliyofanywa na serikali, hivyo nawaasa wadau wote kutumia kongamano hili kujadili na kuangalia namna ya kuboresha mazingira ya ujifunzaji katika progrmu za kimasomo yanayozingatia ubora, usawa na ujumuishi kwa makundi yote,” Amesema.

Amesema kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na UNESCO hivi karibuni, kiwango cha watu wazima wanaojua kusoma, kuandika na kuhesabu ni asilimia 77.89, hali ambayo imeelezwa si mbaya ingawa nchi imerudi nyuma ukilinganisha na miaka ya nyuma.

“Kupitia kongamano hili, watendaji mlitumie kuweka mikakati thabiti ya kuondoa changamoto ya kutojua kusoma, kuandika na kuhesabu nchini, ni dhahiri Taifa lenye watu walioelimika ni rahisi kuleta maendeleo yatakayoweza kubadili maisha ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,” amesema.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Dar es Salaam, Rehema Madenge, akifungua kongamano hilo amesema lengo la maadhimisho hayo ya juma la Elimu ya Watu Wazima ni kujenga uelewa na kutambua changamoto mbalimbali, zinazoikabili tasnia hiyo kwa jamii na dunia kwa ujumla.

“Ni imani yangu tutaweza kubadilisha mitizamo juu ya mipango, uendeshaji, usimamizi, ufuatiliaji na tathmini ya elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi, ili kuendana na dira ya maendeleo ya mwaka 2025,” Amesema.

Amesema pia malengo ya maendeleo endelevu ya mwaka 2030 hasa katika lengo namba nne, ambalo linalenga kuhakikisha vijana na watu wazima wote wanaume na wanawake wanafikia kiwango cha kujua kusoma, kuandika na kuhesababu ifikapo mwaka 2030.

Post a Comment

0 Comments