Ticker

6/recent/ticker-posts

TET, OUT WAASWA KUTUMIA FURSA KUKUZA KISWAHILI NCHINI MALAWI


********************

Serikali imezitaka Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) na Chuo Kikuu Huria (OUT), kuhakikisha inatumia fursa ya kufundisha Kiswahili nchini Malawi kwa lengo la kuikuza lugha hiyo katika nchi za Afrika na dunia kwa ujumla.

Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Caroline Nombo leo Novemba 8, 2022 katika kikao cha pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Malawi Mhe. Humphrey Polepole na wakuu kutoka katika taasisi hizo jijini Lilongwe, nchini Malawi.

Prof Nombo amesema taasisi hizo zina uwezo wa kufanya lugha ya Kiswahili kufahamika kwa katika eneo hilo na kwamba kwa kutumia wataalamu walio nao suala hilo litawezekana na kufanyika kwa haraka.

"Kazi hii ni yenu, nina uhakika mna kila vigezo kuhakikisha Kiswahili kinasambaa hapa Malawi na maeneo mengine duniani," amesema Prof Nombo.

Kwa upande wake Balozi wa Tanzania nchini Malawi, Mhe. Humphrey Polepole amesema tayari kama ofisi ya ubalozi wamefanikiwa kuanzisha ushirikiano huo mzuri ambao utasaidia kukuza Kiswahili na jinsi kitakachoweza kutumika.

Aidha, Mhe. Polepole ameishukuru TET, Chuo Kikuu Huria na Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) kwa kukubali kufanya ushirikiano huo wenye lengo la kuikuza lugha ya Kiswahili na kutoa fursa nchini.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la TET, Prof. Maulid Mwatawala amesema TET ni taasisi bobevu hivyo watatakeleza maelekezo yote ambayo yatasaidia katika kukuza kiswahili na kusaidia Malawi katika eneo la utaalamu wa mitaala, utafiti na uchapaji wa vitabu.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo Kikuu Huria, Prof Elifasi Bisanda ameeleza kuwa fursa hii ya kuanzisha ushirikiano na Malawi ni nzuri ambapo itasaidia kukuza Kiswahili na kufanya wigo nchini hapa na pia kuongeza idadi ya wanafunzi katika vyuo vyao.

Ujumbe wa TET, Chuo Kikuu Huria uko nchini Malawi kwa ziara ya kikazi kwa mwaliko wa Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania nchini Malawi.

Post a Comment

0 Comments