Ticker

6/recent/ticker-posts

DKT. NCHEMBA AMUAHIDI USHIRIKIANO KATIBU MKUU MPYA WIZARA YA FEDHA


Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba akimtambulisha Katibu Mkuu mpya wa wizara hiyo na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba kwa Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Bi. Jenifa Omolo, wakati wa kumkaribisha Katibu Mkuu huyo katika ofisi za wizara jijini Dodoma.


Katibu Mkuu mpya wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba akipokelewa na Mtumishi wa wizara hiyo, Bi. Janeth Mwamwanga, wizarani hapo jijini Dodoma baada ya kuteuliwa na kuapishwa na Raisi wa Jaamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk Samia Suluhu Hassan, wanaoshuhudia ni Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba na Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Bi. Jenifa Omolo.


Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba akizungumza na watumishi wa wizara hiyo wakati wa kumkaribisha Katibu Mkuu mpya na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, jijini Dodoma.


Katibu Mkuu mpya wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba akizungumza na watumishi wa wizara hiyo baada ya kukaribishwa katika ofisi za wizara hiyo jijini Dodoma.

Meza kuu ikiongozwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba na Katibu Mkuu mpya wa wizara hiyo na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba wakiwa kwenye picha ya pamoja na manaibu Katibu Mkuu na wakuu wa idara na vitengo vya wizara hiyo mara baada ya mapokezi ya Katibu Mkuu huyo, jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Fedha na Mipango, Dodoma)

***********************

Farida Ramadhani na Haika Mamuya, Dodoma

Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba amemhakikishia Katibu Mkuu mpya na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El -Maamry Mwamba kwamba Wafanyakazi wa Wizara hiyo watampa ushirikiano wa karibu ili aweze kutekeleza majukumu yake ya kusimamia uchumi wa nchi kwa mafanikio.

Dkt. Nchemba alitoa kauli hiyo wakati wa kikao cha kumkaribisha Dkt. Mwamba katika ofisi za Wizara hiyo jijini Dodoma baada ya kuapishwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ikulu, Chamwino, Dodoma.

“Karibu sana!, uko na timu nzuri, nikuhakikishie kuwa watumishi wote wanafanya kazi kitaalamu na hii ni ishara kwamba ni wabobezi katika majukumu wanayofanya” alifafanua Dkt. Nchemba.

Naye Katibu Mkuu mpya wa wizara hiyo na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El -Maamry Mwamba, aliushukuru uongozi wa Wizara na watumishi kwa kumkaribisha.

Aidha, alisema kuwa teknolojia inabadilika kila wakati hivyo aliwashauri watumishi kujenga tabia ya kujiongezea uwezo wa mambo mbalimbali katika kazi zao ili kuongeza ufanisi na kwenda na wakati.

“Sio kwa mantiki ya kusoma shahada ya uzamili au shahada ya uzamivu, ila kuna zile stadi na vitu kwa kuwa dunia inabadilika kila wakati na kwenda na wakati ni vizuri zaidi” alibainisha Dkt. Mwamba.

Kwa upande wao Manaibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bi. Jenifa Omolo na Bw. Lawrence Mafuru, walisema watampa ushirikiano kwa kushirikiana na wataalam mbalimbali ili kuhakikisha majukumu muhimu ya wizara yanafanyika kwa ufanisi na weledi.

Nao Mhasibu Mkuu wa Serikali, Bw. Leonard Mkude na Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Bw. Athuman Mbutuka walisema kuwa wanaimani na uzoefu na uwezo mkubwa wa kiutendaji aliona nao Katibu Mkuu Mpya wa Wizara hiyo, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba na kwamba ataisaidia nchi kusimamia sera za uchumi ipasavyo.

Dkt. Natu Mwamba, anachukua nafasi iliyoachwa na aliyekuwa Katibu Mkuu na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Emmanuel Tutuba, ambaye ameteuliwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania.

Post a Comment

0 Comments