Ticker

6/recent/ticker-posts

MFUKO WA PAMOJA WA UWEKEZAJI KATI YA TANZANIA NA OMAN KUANZISHWA

Tanzania kwa kushirikiana na Oman zinatarajia kuanzisha Mfuko wa Pamoja wa Uwekezaji (Joint Investment Fund) mwaka huu (2023). Mfuko huo pamoja na mambo mengine, unategemewa kunufaisha sekta za uvuvi, kilimo na madini.

Hayo yamebainishwa katika kikao cha pamoja kati ya Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na Balozi wa Oman nchini, Mhe. Saud bin Hilal bin Saud Al Shidhan kilichofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Balozi Mbarouk amesema kuanzishwa kwa mfuko huo wa pamoja wa uwekezaji ni utekelezaji wa maelekezo ya viongozi wakuu na kuongeza kuwa uanzishwaji wake utasaidia kuinua uchumi wa mataifa yote mawili. “kuanzishwa kwa mfuko huu ni utekelezaji wa maelekezo ya viongozi wetu wakuu ambapo Hati ya Makubaliano (MoU) ya kuanzishwa kwa mfuko huo ilisainiwa mwezi Juni mwaka 2022 kwa lengo la kuinua uchumi wa pande zote mbili na kwa maslahi mapana,” alisema balozi Mbarouk.

Mkataba huo ulisainiwa wakati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipofanya ziara ya kikazi nchini Oman mwaka 2022.

Kwa upande wake, Balozi wa Oman nchini, Mhe. Saud bin Hilal bin Saud Al Shidhan amesema kwa sasa hatua zote zimekamilika na mwaka huu 2023 mfuko huo unategemea kuanzishwa rasmi na kusaidia kuinua biashara na uwekezaji kwa maslahi ya mataifa yote mawili. “mfuko huu utaanza rasmi mwaka huu 2023 na tunategemea uwasaidie kuichumi wafanyabishara na wawekezaji wa mataifa yetu mawili,” alisema Balozi Al Shidhan

Mwezi Juni mwaka 2022, Tanzania na Oman zilisaini Hati sita za Makubaliano katika sekta za nishati, utalii, maliasili, elimu ya juu, mafunzo ya ufundi stadi na makumbusho.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk akizungumza na Balozi wa Oman nchini, Mhe. Saud bin Hilal bin Saud Al Shidhan katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Balozi wa Oman nchini, Mhe. Saud bin Hilal bin Saud Al Shidhan akimfafanulia jambo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk walipokutana kwa mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Kikao cha Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na Balozi wa Oman nchini, Mhe. Saud bin Hilal bin Saud Al Shidhan kikiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk katika picha ya pamoja na Balozi wa Oman nchini, Mhe. Saud bin Hilal bin Saud Al Shidhan


Post a Comment

0 Comments