Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI KUPUNGUZA GHARAMA UPANDIKIZAJI WA MIMBA KUPITIA BIMA YA AFYA KWA WOTE


Na WAF - Dar Es Salaam

Serikali kupitia Wizara ya Afya imejipanga kurejea upya gharama za upandikizaji wa mimba kwa wananchi wenye matatizo ya uzazi na kutopata watoto ili kuwapunguzia mzigo wa gharama kubwa endapo watajiunga na Bima ya Afya kwa wote.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu alipotembelea Taasisi ya Kairuki iliyopo Bunju A jijini Dar Es Salaam ambayo inatoa huduma ya upandikizaji mimba kwa lengo la kuona huduma zinazotolewa kituoni hapo.

Waziri Ummy amesema tatizo la ugumba bado ni kubwa nchini lakini mpaka sasa hakuna takwimu rasmi za kitaifa ila ulifanyika utafiti mdogo ambao unaonesha 30% ya watu wana tatizo la ugumba huku Duniani inakadiriwa kuwa katika kila mahusiano ya wenza wanne, mmoja kati yao anakua na tatizo la kupata watoto.

"Tatizo la kutopata watoto lipo pande zote mbili, upande wa wanaume na wanawake, lakini jamii yetu inachukulia familia isipopata mtoto basi mwanamke ndiyo anaonekana mwenye tatizo. Naamini uwepo wa kituo hiki utasaidia kuondoa fikra potofu". Amesema Waziri Ummy.

Kituo cha upandikizaji mimba cha Kairuki kinatoa huduma hiyo kwa gharama ya kuanzia Shilingi milioni 13 hadi milioni 17 kutegemea na aina ya huduma inayohitajika, hata hivyo Waziri Ummy amesema Serikali itaangalia uwezekano wa kuweka nusu ya gharama hizo katika vifurushi vya Bima ya Afya kwa Wote ili kuweza kuwapunguzia wananchi gharama za kupata huduma hiyo.

“Sisi upande wa Serikali tutaendelea kuwaunga mkono na kuhakikisha kwamba huduma hizi zinatolewa na kuwafikia wengi, tumeelezwa hapa gharama za upandikizaji ni kubwa watanzania wengi hawawezi kumudu, kwahiyo nashukuru mmenileta kipindi hiki tunaenda kuwasilisha muswada wa bima ya afya kwa wote bungeni kwahiyo nitaangalia uwezekano wa bima kuweza kugharamia asilimia 30 au 40 ya baadhi ya huduma zinazohitajika”. Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy ametoa pongezi kwa taasisi ya Kairuki kwa kujenga kituo hicho na kuongeza kuwa ni muhimu sana uwepo wake nchini kwani kitamsaidia mtanzania kupata huduma za upandikizaji wa mimba ndani ya nchi, hivyo amewasisitiza wananchi kwenda kituoni hapo kupata huduma badala ya kutumia fedha nyingi Kwenda nje ya nchi.

Post a Comment

0 Comments