Ticker

6/recent/ticker-posts

WANAFUNZI 63 DIT WAANZA MAFUNZO YA UJASIRIAMALI NA UBUNIFU

Na Mwandishi wetu

Wanafunzi wa kike 63 wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) leo Mei 6,2023 wameanza mafunzo ya siku mbili yanayohusu Teknolojia, ujasiriamali na ubunifu yaliyofanyika katika Ukumbi wa ASA Kampasi Kuu ya Dar es Salaam.

Mafunzo hayo yametolewa na Shirika la Start Hub Afrika linalojihusisha na kutoa elimu kwa wanafunzi wa vyuo Vikuu na vya kati ili wawe na ujuzi wa kutatua changamoto, ujasiriamali pamoja na ubunifu.

Akizungumza baada ya kuwafundisha wanafunzi hao Laura Althaus Mugagga ambaye ni miongoni mwa waanzilishi wa Shirika la Start Hub Afrika amesema DIT ni miongoni mwa Taasisi za Elimu ambazo wanapenda kufanya nao kazi kwa kuwa kwenye masuala ya Teknolojia hapana shaka hivyo hata ukizungumza kuhusu Teknolojia wanafunzi wanalipokea vizuri hivyo Shirika limekuja kuongezea tu.

"DIT inafanya vizuri kiteknolojia na sisi tupo katika harakati za kuhakikisha kuwa tunafanya kazi pamoja ili kuwaongezea wanafunzi chachu ya kuwa wabunifu zaidi maana Teknolojia wanaijua vizuri zaidi."amesema Mugagga.

Aidha amewataka wanafunzi kuwa na ujasiri katika kuendeleza mawazo yao hadi kufikia kwenye zao linaloonekana kwa kutumia ubunifu wao pamoja na Teknolojia.

Naye Magreth Juae mwanafunzi wa DIT mwaka wa tatu wa fani ya Uhandisi umeme ameishukuru DIT kupitia Idara ya mafunzo viwandani kwa kuwawezesha kupata mafunzo haya kwa kuwa yamemuongezea ujuzi.

Amesema. "kupitia training hii nimegundua njia zinazosaidia kutatua changamoto kwenye jamii iliyonizunguka lakini pia nimejifunza hatua za kufuatia ili kutatua changamoto na pia nimepata nafasi ya kuchangamana na wanafunzi wenzangu wenye ujuzi na mtizamo na fikra tofauti".

Naye Debora Elirehema anayesoma fani Uhandisi Ujenzi amesema mafunzo haya ni muhimu kwao kwa kuwa pamoja na kupata ujuzi wamejifunza namna ya kuwasiliana vizuri na kuwa na mawasiliano ya wadau ambao wanawahudumia.

Post a Comment

0 Comments