Ticker

6/recent/ticker-posts

WAFANYABIASHARA WAPYA 35 WASAJILIWA BRELA NDANI YA SIKU 3.


**********************

Na Hamida Kamchalla, TANGA.

JUMLA ya wafanyabiashara wapya 35 wamesajiliwa na Wakala wa Usajili waBiashara na Leseni (Brela) ndani ya siku tatu tu za mwanzo za Maonesho
ya Biashara na Utalii Tanga yaliyofunguliwa rasmi juzi, tayari.

Ofisa Usajili wa Biashara wa Wakala wa Usajili, Julieth Kiwelu, amesema kuwa usajili huo ni uthibitisho unaoonesha kuwa wafanyabiashara wengi wameanza kuelewa umuhimu wa kujali majina ya biashara na kampuni.

Amesema hayo katika mahojiano kwenye Viwanja vya Mwahako Jijini Tanga, kuwa
mwitikio tangu kufunguliwa kwa maonyesho hayo umekuwa mzuri, licha ya mvua kubwa iliyonyesha na kukatiza mahudhurio katika viwanja hivyo.

"Wafanyabiashara wengi wanauliza kuhusu taratibu za usajili hapa
kwenye viwanja vya maonesho, huu ni ushuhuda wa kutambua faida za ofa
hizo za usajili kwa wafanyabiashara na wajasiriamali" amesema.

Kiwelu ameeleza kuwa wakala unatarajia kusajili majina ya biashara
200 ifikapo mwisho wa maonesho hayo ya Biashara na Utalii ifikapo juni 6 ambapo itakuwa ni ndani ya siku 10 za maonesho.

Hata hivyo Kiwelu amesema kuwa BRELA inaelewa matatizo wanayokumbana nayo wafanyabiashara wanaotaka kusajili biashara zao katika mazingira wanayofanyia.


“Ni kweli wafanyabiashara wengi walikuwa wakipata shida kufungua akaunti Brela, hivyo tunatumia fursa hii ya Maonesho ya Biashara kukutana na wateja
wetu na kuwaelekeza namna ya kufungua akaunti na kuwasajili,”
amefafanua.

Amebainisha kuwa kusajili biashara kunaweza kuwapa wamiliki wa biashara hati na vyeti muhimu vya kisheria vinavyothibitisha uhalali wa biashara yao kwa wateja watarajiwa, wawekezaji na washirika.


"Hati hizi na vyeti vinaweza kuongeza imani na uaminifu kwa wale wanaotaka kufanya biashara na kampuni zao, lakini pia kusaidia katika kukuza uaminifu, ambao ni muhimu,"  amesema, na kuongeza, hii inaweza kusaidia biashara yako, kuifanya iwe ya kuvutia zaidi kwa wateja na wawekezaji watarajiwa" amesisitiza.

Kwa mujibu wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara, Wenye
Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA), Mkoa wa Tanga, Jumbe Menye, amesema usajili wa biashara ni hatua muhimu kwa mjasiriamali yeyote anayetaka
kupata mafanikio katika biashara.

"Inaweza kukupa manufaa mbalimbali, kutokana na kuongezeka kwa
uaminifu na uhalali wa kupata programu za usaidizi wa serikali na ulinzi wa haki miliki" amesema Menye ambaye pia ni mmoja wa
waanzilishi wa TCCIA mkoani Tanga.

Post a Comment

0 Comments