Ticker

6/recent/ticker-posts

RC KAGERA AHIMIZA WANANCHI KUTUMIA NISHATI SAFI YA KUPIKIA, AGAWA BURE MITUNGI YA ORYX GAS

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania imegawa mitungi ya 300 pamoja na majiko yake bure kwa wawakilishi wa makundi mbalimbali ya wananchi wa Wilaya zote za Mkoa wa Kagera lengo likiwa kuunga mkono juhudi za Serikali kuhamasisha matumizi safi ya kupikia

.Miongoni mwa makundi ambayo yamepewa mitungi na majiko ya Oryx ni walimu, watumishi wa afya pamoja na Mama Lishe huku Oryx Gas ikiahidi kuendelea kuungalia mkoa huo kwa jicho la pekee kutokana na wananchi wake kuendelea kutunza mazingira na hasa miti ya asili.

Ugawaji wa mitungi huo umeratibiwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera ukisimamiwa na Mkuu wa mkoa huo Fatma Mwasa.

Akizungumza wakati wa ugawaji mitungi hiyo Mkuu wa Mkoa Fatma Mwasa amesema ni vema wananchi wa mkoa huo wakaendelea kutunza misitu kwa kutokata miti hivyo na njia ya kutunza misitu ni kutumia nishati safi ya kupikia ikiwemo gesi.

Amesema Serikali ya Mkoa wa Kagera imeendelea kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia na kuachana na matumizi ya kuni na mkaa huku akisisitiza wananchi wa Kagera huo kutoharibu misitu kwa kukata miti na badala yake wameendelea kuitunza na kuhifadhi misitu.

Aidha ameipongeza Kampuni ya Oryx Gas kwa kutoa mitungi ya gesi kwa wawakilishi wa makundi mbalimbali wa mkoa huo."Nawashukuru Oryx kwa kuuangalia Mkoa huu Kagera lakini niendelee kuwasisitiza wananchi acheni kukata miti kwa ajili ya kuni na mkaa."

Mwasa ametumia nafasi hiyo kuelezea faida lukuki za kutumia nishati safi ya kupikia ikiwemo ya usalama wa afya kwani matumizi ya kuni na mkaa yana athari za kiafya.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Oryx Gas Tanzania Araman Benoite, Antonia Kilama amesema lengo la kampuni hiyo kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akihimiza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

"Kampuni yetu ya Oryx Gas tumekuwa tukiunga mkono juhudi za Serikali ua Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambayo imeweka lengo la kufikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2030.

"Oryx Gas ina nia ya dhati kusaidia Watanzania hasa wanawake ambao wamekuwa wakiathirika zaidi na matumizi ya kuni na mkaa, hivyo tumekuwa tukigawa mitungi ya gesi na majiko yake bure kwa wananchi wa mikoa mbalimbali na leo tuko hapa Kagera."

Awali akizungumza na waandishi wa habari Meneja Masoko wa Oryx Gas Tanzania Peter Ndomba amesema hadi sasa kampuni hiyo imeshagawa bure mitungi ya gesi na majiko yake 10, 000 katika mikoa mbalimbali nchini na hivyo kugusa makundi yote kwenye jamii.

Pia amesema kwa Mkoa wa Kagera watauangalia kwa jicho la aina yake ni mkoa ambao wamefanikiwa kuhifadhi misitu hivyo njia pekee ni kuwaunga mkono kwa vitendo kwa kuwahamasisha kutumia nishati safi ya kupikia kama sehemu ya kulinda na kuhifadhi misitu ya asili.
Mkuu wa mkoa akimkabidhi mtungi mmoja wa wanufaika wa msaada toka Oryx, kulia ni mkuu wa wilaya ya Bukoba

Wananchi wakisikiliza hotuba ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera Fatma Mwasa wakati wa tukio la ugawaji wa mitungi ya Oryx Gas na majiko yake bure kwa wananchi wa makundi mbalimbali ya Mkoa huo

Timu ya Oryx Gas wakitoa mafunzo ya matumizi salama ya nishati ya gesi ya kupikia ikiongozwa na Meneja wa Masoko Peter Ndomba(katikati)
Wanakagera wakipokea mafunzo ya matumizi ya nishati safi na salama ya kupikia kabla ya kupewa mitungi ya gesi na majiko yake bure kutoka kampuni ya Oryx Gas

Post a Comment

0 Comments