Ticker

6/recent/ticker-posts

DKT. RWEZIMULA AHIMIZA USHIRIKI KATIKA MAADHIMISHO YA KITAIFA JUMA LA ELIMU YA WATU WAZIMA


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Franklin Rwezimula ,akitembelea mabanda ya maonesho katika juma la Elimu ya Watu wazima linalofanyika katika Viwanja vya Maili Moja wilaya ya Kibaha mkoani Pwani ili kujionea huduma zinazotolewa kuelekea Kilele cha Maadhimisho ya Kitaifa ya Juma hilo, Oktoba 13, 2023.

...............

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Franklin Rwezimula leo Oktoba 11, 2023 amewahimiza Wananchi kutoka mkoani yote kutumia vema Maadhimisho ya Kitaifa ya Juma la Elimu ya Watu Wazima, kuona mafanikio ya program mbalimbali za Kielimu zinazotapelewa na Taadidi hiyo pamoja na Taasisi za Elimu ya Juu, Vyuo vya Kati na vya Ufundi.

Dkt. Rwezimula ametoa rai hiyo leo Oktoba 11, 2023 wakati akitembelea mabanda ya maonesho katika juma la Elimu ya Watu wazima linalofanyika katika Viwanja vya Maili Moja wilaya ya Kibaha mkoani Pwani ili kujionea huduma zinazotolewa kuelekea Kilele cha Maadhimisho ya Kitaifa ya Juma hilo, Oktoba 13, 2023.

‘’nimefarijika kukuta Taasisi za Elimu ya Juu na Vyuo vingine ambavyo vinatoa mafunzo yanayohusu Elimu ya Watu Wazima wako hapa, lakini pia nimekutana na Vikundi vya Watu Wazima ambao wamenufaika na program mbalimbali zinazoendeshwa na Taasisi yetu ya Elimu ya Watu Wazima’’ alisema Dkt. Rwezimula.

Aidha Dkt. Rwezimula amefurahishwa kukutana na Vikundi vya Vijana wa Kike, ambao wamepewa fursa ya kurudi shuleni kupitoa Waraka wa Elimu namba 3 wa 2021 kuendelea na masomo, baada ya kukatiza kwa sababu mbalimbali.

‘’Mtakumbuka Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alituelekeza Wizara ya Elimu, kuandaa mpango Maalum wa kuwarudisha vijana shuleni waweze kufaidika na fursa za masomo, na sasa vijana wengi wamerudi katika vituo mbalimbali’’. Alieleza Dkt. Rwezimula.

Naibu Katibu Mkuu huyo amevipongeza Vikundi vya Wanawake Watu Wazima ambao wamendelea kutumia kikamilifu fursa zinazotolewa za kupata elimu bila kujali umri walionao, ikiwa ni pamoja na kuyatumia maarifa katika kuzalisha bidhaa mbalimbali kwa ajili ya kuwahudumia Watanzania.

‘’Nimefurahi kukutana na Vikundi vya wakinamama ambao walikuwa hawajui kusoma na kuandika, lakini kulingana na program ambazo zimeandaliwa wameweza kusoma lakini pia wameweza kuanzisha shughuli mbalimbali za kujipatia kipato’’. Alinena Dkt. Rwezimula.

Akizungumza kuhusu mafanikio aliyoyapata Siri Kibinda, Mwanamke Mjasiriamali kutoka Halmashauri ya wilaya ya Kibaha, ambaye ni mnufaika wa mafunzo kupitia Mpango wa Uwiano kati ya Elimu na Jamii (MKEJA) amesema kwamba Mpango huu umemuwezesha kujifunza na kumudu kikamilifu shughuli za ujasiriamali.

‘’Nimepata ujasiriamali kupitia darasa la MKEJA, darasa hili limeninufaisha sana kwa sababu nilikuwa sijui kusoma wala kuandika, lakini sasa hivi ninajua kusoma na kuandika, hata lebo za bidhaa zangu nimeziandika mwenyewe’’ alibainisha Kibinda.

Nae Ruth Waluye Mwanafunzi katika Kituo kilichopo Shule ya Sekondari Tumbi, amesema kupitia Mradi wa Kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP) unawawezesha Wasichana wengi kurudi masomoni hivyo wanaamini watatimiza malengo yao kwani watapata elimu na mafunzo ya amali yanayowajengea ujuzi.

‘’Elimu tuliyoipata kwenye somo la Kemia na stadi za Maisha tumeweza kutengeneza bidhaa za sabuni zetu kwa ajili ya kukidhi mahitaji yetu. Nikimaliza mitihani yangu mwezi Novemba, nikirudi mtaani sitokuwa na shida ya kutafuta ajira, nitajiajiri na kazi za ujasiriamali ili nijipatie kipato’’ alisema Ruth.

Kuelekea Kilele Cha Maadhimisho ya Kitaifa ya Juma la Elimu ya Watu Wazima Dkt. Rwezimula amewataka Wananchi kutumia fursa hiyo kutembelea maonesho kujifunza masuala yahusuyo Elimu na kijamii, huku akisisitiza kwamba Elimu haina mwisho.

Post a Comment

0 Comments