Ticker

6/recent/ticker-posts

WADAU WA UNUNUZI WASHAURIWA KUZINGATIA UADILIFU, UAMINIFU NA HAKI

Serikali imewapa changamoto wadau wa Sekta ya ununuzi wa umma kuhakikisha wanazingagtia misingi ya uadilifu, uaminifu na haki katika michakato ya ununuzi wa umma ili kuiwezesha Serikali kupata thamani ya fedha.

Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba katika hotuba yake iliyosomwa na Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Wizara ya Fedha, Bw. Moses Dulle wakati wa kufunga mafunzo ya siku mbili juu ya moduli ya uwasilishaji wa malalamiko/rufaa kwa njia ya kieletroniki yamendaliwa na Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa mikoa ya Dar es Salaam, Tanga Morogoro na Pwani, Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Mwamba amesema umuhimu wa mafunzo kuhusu moduli ya uwasilishaji wa malalamiko/rufaa kwa njia ya kieletroniki umechagizwa na mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayoendelea duniani hususan kutungwa upya kwa Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023 na kuruhusu hatua za mageuzi kuchukuliwa.

“Kutungwa upya kwa sheria ya ununuzi wa umma 2023 kumesaidia kuongeza ufanisi, haki, uwazi na uwajibikaji katika ununuzi wa umma,” alisema Dkt. Mwamba

Hotuba yake imeongeza kuwa aslimia 70 ya matumizi ya Serikali huelekezwa katika ununuzi wa umma ambapo kwa kutumia mfumo mpya, uwazi na uwajibikaji utaisaidia serikali kupata thamani halisi ya fedha katika miradi yake.

Pamoja na mambo mengine, Katibu Mkuu ameielekeza Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) ili kuiwezesha kufikia mlengo ya kutoa uelewa wa moduli ya uwasilishaji wa malalamiko/rufaa kwa njia ya kieletroniki kwa wadau wa ununuzi na kujenga uelewa wa pamoja.

Awali, Mwenyekiti wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma, Mhe. Jaji Mstaafu Sauda Mjasiri amesema kuwa mafunzo hayo yaatakuwa endelevu nakuwawezesha wadau wa sekta ya ununuzi nchini kuwa na uelewa wa pamoja.

“Kupitia mafunzo haya ya siku mbili mada mbalimbali zimewasilishwa hususan moduli ya uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko au rufaa……….kutokana na mwitikio ulioonekana umeonesha nia njema ya kuwafikia wadau wengi na kuongeza uelewa na ufanisi katika sekta ya ununuzi nchini,” amesema Jaji Sauda.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), Bw. James Sando alisema kuwa Mamlaka ya Rufani itaendelea kushirikiana na PPRA kusimamia zoezi la kutoa mafunzo ya mfumo mpya wa kuwasilisha na kushughulikia malalamiko/rufaa kwa njia ya kieletroniki (Complaint and Appeal Management) ili kuwawezesha wengine kujua jinsi ya kutumia moduli hii ya malalamiko.

Bw. Sando ameongeza kuwa PPAA itaendelea kuzielimisha taasisi nunuzi na wazabuni wa kanda nyingie kuhusu mfumo huu mpya hususan Moduli ya kuwasilisha na kushughulikia malalamiko/rufaa kieletroniki.

Mafunzo hayo yalianza tarehe 29 – 30 Mei, 2024 yalitolewa kwa taasisi nunuzi, wazabuni pamoja na mawakili yamelenga kuwajengea wadau hao uelewa kuhusu mfumo mpya wa kuwasilisha na kushughulikia malalamiko/rufaa kwa njia ya kieletroniki (Complaint and Appeal Management) ili kuwawezesha wengine kujua jinsi ya kutumia moduli hii ya malalamiko.

Post a Comment

0 Comments