Ticker

6/recent/ticker-posts

MWANASOKA WA AFGHANISTAN AFARIKI DUNIA BAADA YA KUANGUKA KUTOKA KWA NDEGE YA MAREKANI


Mamlaka ya Afghanistan imethibitisha kwamba mwanasoka kijana alifariki dunia baada ya kujaribu kuondoka nchini humo kwa kudandia ndege ya jeshi la Merekani na kuanguka uwanja wa ndege wa Kabul.

Zaki Anwari, 19, alikuwa ameichezea timu ya taifa ya vijana ya Afghanistan.

Maelezo zaidi ya ni lini alifariki dunia bado hayajawekwa wazi.

Tangu Taliban kuteka nchi ya Afghanistan, maelfu ya watu wamejitokeza kwenye uwanja wa ndege wa Kabul, wakati ambapo nchi za Magharibi zinakimbilia kuhamisha raia wao na wenzao wa Afghanistan.

Picha ziliibuka Jumatatu zikionyesha mamia ya watu wakikimbia kufuata ndege ya jeshi la anga la Marekani wakati ikishuka kwenye barabara ya kupaa.

Watu wengine walionekana wakishikilia upande mmoja wa ndege.

Ripoti za vyombo vya habari vya eneo zasema kwamba watu wasiopungua wawili waliuawa baada ya ndege hiyo kupaa.

Kikosi cha anga cha Marekani pia kimethibitisha kuwa mabaki ya binadamu yalipatikana katika vifaa vya kutua vya ndege baada ya kuwasili Qatar.


Chanzo: BBC Swahili

Post a Comment

0 Comments