Ticker

6/recent/ticker-posts

DKT.HASHIL AFUNGUA KONGAMANO LA TATU LA WAKUFUNZI WA KAIZEN


...........................................

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Hashil T. Abdallah amefungua Kongamano la tatu la wakufunzi la KAIZEN lilioandaliwa na Kitengo cha KAIZEN kilichopo Wizara ya Viwanda na Biashara.

Akifungua mkutano huo leo tarehe 20 Oktoba, 2021 wenye kauli mbiu inayosema “KAIZEN kwa Tanzania ya Viwanda na Maendeleo Jumuishi” Dkt. Hashil Abdalllah amesema anaishukuru serikali ya Tanzania kwa kuwezesha Kongamano la KAIZEN lililofanyika mwaka huu nchini Tanzania, pia ameishukuru serikali ya Japan kupitia JICA kuendelea kufadhili mradi huu.

Dhamira ya uongozi wa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan ni kukuza uchumi wa nchi kupitia sekta ya Viwanda na Biashara ambayo itasaidia kukuza pato la taifa na ajira kwa watanzania.

Dkt. Hashil ameongeza kwa kusema kuwa “Falsafa ya KAIZEN inasaidia kuongeza Tija, Ufanisi, Ubora na pia kuongeza fulsa za ajira, Falsafa hii imesaidia kubadilika kwa mtazamo na fikra kwa wamiliki wengi wa Viwanda inayopelekea kukua kwa biashara zao” Amesema Dkt. Hashil.

Ameongeza kwa kusema kuwa viwanda 135 tu ndio vilivyofikiwa na KAIZEN hivyo amewataka wakufunzi walioshiriki kongamano hili kujadiliana kwa kina kuona namna bora ya kuvifikia viwanda vingi zaidi vilivyopo nchini.

Dkt. Hashil amesema kuwa Wizara imejipanga Kuendeleza miundombinu ya msingi na saidizi ya maeneo ya uwekezaji kongano za viwanda na huduma ya viwanda kwa wawekezaji na wajasiriamali, Kusimamia uanzishwaji wa maeneo maalum ya kibiashara (trading hubs) hususan kwa maeneo ya mipakani, Kusimamia utekelezaji wa miradi ya kielelezo iliyopo katika Mpango wa Maendeleo wa tatu, Kuweka mkazo na msisitizo katika kukuza na kuchochea viwanda vidogo na vya kati (SMEs) vinavyotumia teknolojia rahisi na ya kisasa vijijini na mijini, Kuboresha kanzidata kwa ajili ya kupata takwimu sahihi za viwanda nchini, Kuimarisha utafiti na matumizi yake, Kufufua Viwanda Vilivyobinafsishwa, upanuzi na ukarabati wa viwanda vilivyopo na kuchochea uwekezaji/uanzishwaji wa viwanda vipya, Uendelezaji na uwekezaji katika maeneo maalum ya uwekezaji na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje, Kulinda viwanda na biashara za ndani dhidi ya ushindani usio wa haki, Kudhibiti ubora na viwango vya bidhaa, Kujenga mifumo imara ya soko la ndani na kuhamashisha utafutaji na utumiaji wa fursa nafuu za masoko, Kupanua na kuboresha mahusiano na ushirikiano na Taasisi za sekta binafsi, tukitambua kuwa, kisera, sekta binafsi ndio wajenzi, wamiliki na waendelezaji wa sekta ya viwanda nchini;

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Viwanda, Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Lugano Wilson Amesema kuwa kama ilivyo katika nchi nyingi duniani, ni jukumu la Serikali kuweka mazingira bora ya biashara ambayo yatachangia kuifanya nchi kuwa ya ushindani zaidi katika uzalishaji, biashara na shughuli nyinginezo za kiuchumi ili kutambuliwa kama nchi ya ubora, ufanisi na tija.

Dkt. Wilson ameongeza kwa kusema kuwa, Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikisha wadau kutoka sekta Binafsi na sekta ya Umma inaendeleza sekta ya viwanda kulingana na malengo ya mipango mipana ya maendeleo ya nchi yetu.

Amesma kuwa “Wizara inasimamia utekelezaji wa sera za kuendeleza sekta za viwanda, biashara na masoko. Pia, Wizara iko katika hatua za kukamilisha Sera ya Taifa ya Ubora (NQP) ambapo rasimu yake itawasilishwa na kujadiliwa katika kongamano hili” Amesema Dkt. Lugano.

Vile vile amesema kuwa uhamasishaji wa matumizi ya falsafa ya KAIZEN ni miongoni mwa juhudi za Wizara za kuijengea uwezo sekta ya viwanda nchini katika harakati za kutekeleza Sera ya Maendeleo Endelevu ya Viwanda (1996) na mkakati wake (IIDS 2011).

Juhudi hizi zina malengo mapana ya kuijengea uwezo sekta binafsi katika uendelezaji wa viwanda.

Naye mwakilishi wa JICA nchini Tanzania ndugu Chinochiro Kato amesema kuwa wakufunzi wa KAIZEN ni muhimu sana kwa maendeleo ya Viwnda nchini Tanzania hivyo amefurahishwa kwa waandaaji kuandaa Kongamano hili liloshirikisha wadau kutoka mikoa mbalimbali nchini.

Naye mwakilishi kutoka shirikisho la wenye Viwanda nchini Tanzania (CTI) ndugu Neema Mhando Ameipongeza wizara ya viwanda na biashara kwa kutekeleza falsafa ya KAIZEN kwa vitendo na kwa mafanikio makubwa na pia kupanua wigo wa utekelezaji wa mradi huu kwa kuongeza mikoa minne zaidi katika kuhakikisha nchi nzima inafikiwa na falsafa hii ambayo imesaidia kuongeza ufanisi na tija Viwandani.

Kongamano hili limehudhuriwa na wakufunzi kutoka Mikoa ya Dodoma, Mwanza, Singida, Kilimanjaro, Arusha, Dar es salaam, Tabora na Mbeya.

Post a Comment

0 Comments