Ticker

6/recent/ticker-posts

PROFESA MKENDA AHIMIZA MATUMIZI YA MBOLEA KWA KILIMO CHENYE TIJA


Waziri wa Kilimo Prof Adolf Mkenda akisalimiana na Mkurugenzi wa Mamlaka ya udhibiti wa mbolea nchini(TFRA) Dkt. Stephen Ngailo mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Majimaji Songea ambapo maadhimisho ya siku ya mbolea duniani yamefanyika


Waziri wa Kilimo Prof. Adolf Mkenda akisikiliza maelezo kutoka kwa wataalam wa taasisi ya uthibiti wa mbegu bora (TOSCI) alipotembelea banda lao, wakati wa maadhimisho ya siku ya mbolea duniani, yaliyofanyika katika uwanja wa Majimaji Songea Mkoa wa Ruvuma


Waziri wa Kilimo, Prof. Adolf Mkenda akisikiliza maelezo ya aina bora za mbolea bora kutoka kwa Bw. Michael Sanga meneja wa TFRA kanda ya njuanda za juu kusini, wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya mbolea duniani, uwanja wa majimaji Songea mkoa wa Ruvuma.

..............................................

WAZIRI wa Kilimo Profesa Adolf Mkenda,amehimiza matumizi ya mbolea katika shughuli za kilimo ili kuleta ufanisi na kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara mashambani.

Waziri Mkenda amesema hayo jana,wakati akifunga maadhimisho ya siku ya mbolea Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa michezo wa majimaji mjini Songea.

Amesema,licha ya wakulima hapa nchini kuzalisha kwa wingi,lakini matumizi ya mbolea katika kilimo hayazidi tani 9 badala yake kiasi cha mbolea kinachotumika katika shughuli za kilimo kwa ncji mzima ni kati ya tani 4 hadi 5 kwa mwaka.

Kwa mujibu wa Profesa Mkenda,pamoja na ukweli kwamba wakulima ndiyo wazalishaji wakubwa wa chakula,hata hivyo bado kuna changamoto zinazosababisha wakulima kuwa na tija ndogo ya uzalishaji.

Waziri Mkenda ametaja changamoto hizo ni pamoja na matumizi madogo na yasio sahihi ya mbolea, yanayotokana na utumiaji mbolea pasipo kutambua afya ya udongo wa eneo husika na matumizi ya mbegu zenye viwango vidogo vya ubora.

Changamoto nyingine ni maogonjwa ya mimea na mabadiliko ya tabia ya nchi yanayosababisha ukame,mafuriko na milipuko ya visumbufu vya mimea pamoja na matumizi ya zana duni za kilimo unaofanya gharama za uzalishaji kuwa kubwa.

Katika kukabiliana na changamoto hizo Profesa Mkenda amesema, serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imechukua hatua mbalimbali ikiwemo kuruhusu wafanya biashara kuagiza mbolea kwa bei ya soko na kuuza kwa bei shindani ili wakulima wengi wapate mbolea kwa bei atakayoimudu.

Aidha amesema, Serikali imeendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza kwenye ujenzi wa viwanda vya kuzalisha mbole hapa nchini ili kuhakikisha mbolea inapatikana kwa bei rafiki na kwa wakati ambapo wawekezaji kadhaa wameshajitokeza.

Amesema, jitihada hizo za Serikali zinalenga kumuwezesha mkulima kupata mbolea kwa bei nafuu na hivyo kuongeza matumizi ya viinilishe vya mimea vitokanavyo na mbolea kutoka wastani wa kilo 19 hadi kilo 50 za virutubisho hivyo kwa hekta, kama ilivyoazimiwa na wakuu wa nchi za Afrika katika mkutano uliofanyika Abuja Nchini Nigeria mwaka 2007.

Katika hatua nyingine Profesa Mkenda amesema, katika msimu wa kilimo 2021/2022 ulioanza mwezi Oktoba tayari jumla ya tani 141,725.7 za mbolea zimeshaingizwa nchini na tani 117,900 ni bakaa yam waka 2020/2021.

Amesema, hatua hiyo inafanya upatikanaji wa mbolea nchini kufikiwa jumla ya tani 283,625.7 za mbolea kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya wa kilimo na tani 21,900 zinarajiwa kuingizwa mwezi mwezi huu.

Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Brigadia Jenerali Wilbert Ibuge ameishukuru wizara ya kilimo kupitia mamlaka ya udhiti wa mbolea Tanzania(TFRA)kufanya maadhimisho ya wiki ya mbolea mkoani Ruvuma.

Amesema, mkoa wa Ruvuma ni kati ya mikoa inayozalisha kwa wingi chakula na zaidi ya asilimia 87 ya wakazi wake wanategemea shughuli za kilimo kuendesha maisha yao ya kila siku.

Awali Mwenyekiti wa Bodi ya TFRA Profesa Stephen Ngailo amesema, mamlaka imeendelea kuimarisha mifumo ya udhibiti wa mbolea ili kuhakikisha wakulima wanapata mbolea bora na kwa wakati.

Amesema, tangu 2016/2017 hadi Septemba 2021 jumla ya mbolea zilizosajiliwa zilikuwa 356 na hivyo kuongeza mbolea zilizohakikiwa kufaa katika urutubishaji wa udongo.

Aidha ameeleza kuwa, matumizi ya mbolea yameongezeka na hivyo kuongeza uzalishaji ambapo ametolea mfano mwaka 2015/2016 matumizi ya mbolea yalikuwa tani 296,036 na mwaka 2021 matumizi yameongezeka hadi kufikiwa tani 475,870.

Post a Comment

0 Comments