Ticker

6/recent/ticker-posts

BENKI YA TCB YATOA MSAADA WA MADAWATI SHULE YA MSINGI KOMBOA

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya Mbinga mkoani Ruvuma Samwel Komba wa pili kushoto,akipokea moja ya madawati 50 kutoka kwa Mkurugenzi wa Ukaguzi wa ndani wa Benki ya Biashara Tanzania(TCB) Sosthenes Nyenyembe yaliyotolewa na Benki hiyo kwa ajili ya wanafunzi wa shule ya Msingi Komboa kijiji cha Ruanda wilayani Mbinga,kushoto aliyesimama ni Meneja wa Benki ya TCB Tawi la Songea Richard Chacha na wa kwanza kulia Diwani wa Kata ya Ruanda Deogras Mwingira.
Mkurugenzi wa Ukaguzi wa ndani Benki ya Biashara Tanzania(TCB)Sosthenes Nyenyembe wa tatu kulia,Meneja Uhusiano kwa wateja wa Benki hiyo Gloria Mutta katikati,Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya Mbinga Samwel Komba wa kwanza kushoto na Meneja wa Bebki ya TCB Tawi la Songea Richard Chacha wa pili kushoto wakikate utepe kabla ya Benki hiyo kukabidhi msaada wa madawati 50 yenye thamani ya Sh.milioni 4.3 kwa shule ya msingi Komboa kata ya Ruanda wilayani Mbinga,wa pili kulia Diwani wa kata ya Ruanda Deogras Mwingira.
Mkurugenzi wa Ukaguzi wa ndani wa Benki ya Biashara Tanzania(TCB) Sosthenes Nyenyembe wa kwanza kushoto na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya Mbinga Samwel Komba wa pili kulia na Diwani wa kata ya Ruanda Deogras Mwingira wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Komboa baada ya Benki ya TCB kukabidhi msaada wa madawati 50 yenye thamani ya Sh.milioni 4.3 kwa shule hiyo.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya Mbinga Samwel Komba kushoto,akipokea Kalenda ya mwaka 2022 kutoka kwa Mkurugenzi wa Ukaguzi wa ndani wa Benki ya Biashara Tanzania(TCB)Sosthenes Nyenyembe aliyevaa suti wakati wa hafla ya kukabidhi madawati 50 yenye thamani ya Sh.milioni 4.3 kwa shule ya msingi Komboa kata ya Ruanda wilayani Mbinga yaliyotolewa na Benki hiyo.


**********************
Na Muhidin Amri,
Mbinga

BENKI ya Biashara Tanzania(TCB),imetoa msaada wa madawati 50 yenye thamani ya Sh.4,300,000 kwa shule ya msingi Komboa iliyopo kijiji cha Ruanda Halmashauri ya wilaya Mbinga mkoani Ruvuma.


Hii ni mara ya tano kwa Benki hiyo kutoa misaada kwa shule mbalimbali za msingi na Sekondari mkoani Ruvuma, ikiwa ni mpango wake wa kurejesha faida kwa jamii tangu ilipoanzishwa miaka kadhaa iliyopita.


Akizungumza mara baada ya kukabidhi msaada huo, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani wa Benki ya Biashara Tanzania Sosthenes Nyenyembe alisema, Benki ya TCB inatazama changamoto zilizopo katika sekta ya elimu kama moja ya vipaumbele vyake vikuu,kutokana na ukweli kwamba elimu ndiyo ufunguo wa maendeleo sio tu ya mtu mmoja mmoja bali pia kwa Taifa.


Nyenyembe alisema, Benki ya TCB itaendelea kutoa misaada kwa jamii katika sekta mbalimbali hususani elimu na afya kulingana na mahitaji na changamoto zinazoikabili jamii hapa nchini.


Hata hivyo alisema, wazazi na walezi ndiyo wenye wanajukumu kubwa la kuhakikisha watoto wanapata elimu nzuri, kwani maisha bila elimu ni sawa na kukosa mwanga katika maisha.


Amewataka,kuwekeza sana kwenye elimu ya watoto wao,kwani ndiyo ufunguo,mwanga na njia ya kufikia malengo yao ya baadaye badala ya kuwarithisha mila potofu ambazo hazitawasaidia watoto katika maisha yao.


Aidha alisema,Benki ya TCB inatoa huduma ya mikopo kwa wastaafu ambapo alieleza kuwa faida ya mkopo huo ni pale ikitokea mstaafu amefariki Dunia familia ya marehemu haitosumbuliwa kulipa mkopo huo.

Amewaomba wananchi wa wilaya ya Mbinga na mkoa wa Ruvuma, kuiunga mkono Benki hiyo kwa kufungua akaunti,kupata mikopo na kutumia huduma mbalimbali kwa ajili ya shughuli zao za kiuchumi.


Afisa Mtendaji wa kijiji cha Ruanda Idrissa Machumu alisema, shule hiyo ina zaidi ya wanafunzi 301 ambao wanahitaji madawati 182 na yaliyopo kwa sasa ni 50.

Pia alitaja changamoto nyingine ni vyoo na nyumba za walimu hali inayofanya walimu kukaa mbali na eneo la shule, hivyo kushindwa kutekeleza majukumu yao katika suala zima la ufundishaji wa wanafunzi madarasani.


Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya Mbinga Samwel Komba, ameishukuru Benki ya TCB kwa msaada huo ambao unakwenda kupunguza changamoto ya madawati kwa wanafunzi wa shule ya Msingi Komboa.


Komba alisema,Halmashauri ya wilaya Mbinga ina uhitaji mkubwa wa madawati ambapo kwa shule za msingi 164 zilizopo zinahitaji jumla ya madawati 21,782 na yaliyopo ni 19,861.

Komba ambaye ni Afisa elimu ya msingi wa Halmashauri hiyo,amewaomba wadau mbalimbali kusaidia sekta ya elimu ambayo bado inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo madawati,nyumba za walimu,matundu ya choo na madawati ambayo ili kumaliza kunahitajika nguvu za pamoja badala ya kuichia Serikali pekee yake.


Aidha,aliipongeza Benki hiyo kwa namna ilivyojipambanua katika kusaidizi kutatua changamoto katika sekta ya elimu na afya nchini na kuwataka wanafunzi wa shule hiyo kutunza madawati hayo ili yaweze kudumu na kuleta tija iliyokusudiwa.


Alisema,kwa ujumla safari ya elimu ni ngumu na iliyojaa changamoto nyingi kwa wanafunzi,wazazi na hata walimu hivyo ni wanapaswa kuthamini michango inayotolewa na wadau mbalimbali ili itumike kwa muda mrefu.

Post a Comment

0 Comments