Ticker

6/recent/ticker-posts

KAMATI YA BAJETI BARAZA LA WAWAKILISHI ZANZIBAR YASHAURI VIKUNDI VYA WANUFAIKA WA TASAF BARA NA VISIWANI KUUNGANA


Ali Suleiman Ameir Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar akizungumza na wanufaika wa TASAF wa Kiwalani Minazi Miwili wilayani Ilala, katika Jiji la Dar es Salaam wakati kamati hiyo ilipotembelea miradi mbalimbali ya wanufaika nakujionea shughuli mbalimbali leo.


Ali Suleiman Ameir Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar pamoja na wajumbe wenzake wakiangalia mradi wa kutengeneza vitofali vya sakafu akipokagua miradi ya wanufaika wa TASAF wa Kiwalani Minazi Miwili wilayani Ilala, katika Jiji la Dar es Salaam wakati kamati hiyo ilipotembelea miradi hiyo leo.


Msimamizi wa mradi wa kufyatua vitofali Bw. Eric Silvanus Mwang'ombe akitoa maelezo kwa wajumbe wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar wakati walipowatembelea wanufaika wa TASAF wa Kiwalani Minazi Miwili wilayani Ilala, katika Jiji la Dar es Salaam wakati kamati hiyo ilipotembelea miradi


Ali Suleiman Ameir Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar akiangalia mradi wa ujenzi wa Kizimba katika shule ya sekondari unaoendeshwa na wanufaika wa TASAF wa Kiwalani Minazi Miwili wilayani Ilala, katika Jiji la Dar es Salaam wakati kamati hiyo ilipotembelea miradi


Mh.Ali Suleiman Ameir Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar akiangalia bidhaa mbalimbali zilizotengenezwa na wanufaika wa TASAF wa Kiwalani Minazi Miwili wilayani Ilala, katika Jiji la Dar es Salaam wakati kamati hiyo ilipotembelea miradi mbalimbali ya wanufaika hao leo.


Baadhi ya wanufaika wakimsikiliza Mh.Ali Suleiman Ameir Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar alipokuwa akizungumza nao leo.

............................................

KAMATI ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, imeshauri kuwepo kwa utaratibu wa vikundi vya wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya masikini (TASAF), kutoka Bara na visiwani kuungana ili wabadilishane uzoefu.

Ushauri huo ulitolewa jana na Mwenyekiti wa kamati hiyo Mh. Ali Suleiman Ameir, wakati wa ziara ya kamati hiyo ya kuwatembelea wanufaika wa TASAF wa Minazi Miwili wilayani Ilala, katika Jiji la Dar es Salaam.

Alieleza kutokana na mafanikio waliyoyapata wanufaika hao, hapana budi waungane na wenzao kutoka Zanzibar ili kushirikiana na kubadilishana uzoefu katika matumizi ya ruzuku wanazopata.

Alisisitiza kwamba mafanikio waliyoyapata wanufaika hao ni hatua nzuri katika kutafsiri dhamira ya kuanzishwa kwa mpango wa TASAF.

Aliwahimiza wanufaika wote waliovuka hatua ya kuwa kaya masikini kuhakikisha wanajiondoa kwa hiari ili wengine wenye uhitaji wanufaike.

Akijibu changamoto zilizowasilishwa na wawakilishi wa wanufaika hao, Mwenyekiti huyo aliahidi kuzungumza na wahusika ili kuona namna ya kukabiliana nazo.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mjumbe wa Kamati hiyo, Mh. Issa Gavu, aliwasisitiza wanufaika kusimamia msingi huo wa mafanikio na kuhakikisha hawarudi katika wimbi la kaya masikini.

Alieleza TASAF ni kuelelezo sahihi cha muungano kwani changamoto zinazozungumzwa bara ndizo zilizopo visiwani.

Naye, Mnufaika wa TASAF, Mwashabani Binyango, alisema kutokana na mpango huo kwa sasa ana uhakika wa milo mitatu na anasomesha wanawe bila changamoto.

Alibainisha hata nyumba yake haikuwa na sakafu, lakini kutokana na ruzuku ya fedha hizo kwa sasa ameweka saruji katika sakafu.

Mnufaika mwingine, Fatuma Kiswamba, alieleza elimu ya vikoba waliyopewa na TASAF imemwezesha sasa kuwa na kikundi ambacho hukopeshana na hivyo kujikimu kwa mahitaji mbalimbali.

Alisema kwa sasa ana uhakika wa mlo kamili na kipato chake kinakidhi mahitaji ya familia yake.

Ofisa Mtendaji wa Mtaa wa Minazi Miwili, Oliver Makweta, alibainisha kwamba kupitia ruzuku wanazopata wanufaika hao wamejiunga katika kikundi na wanashirikiana katika kufanya miradi kadhaa.

Alitaja moja ya miradi hiyo ni kutengeneza matofali na hivyo kuwawezesha kukidhi mahitaji yao.

Aliongeza kwamba kupitia kikundi hicho wamekuwa wakikopeshana na kulipa kwa utaratibu maalumu, utaratibu ambao umeinua maisha ya wengi wao.

Post a Comment

0 Comments