Ticker

6/recent/ticker-posts

PROGRAMU YA TOBOA NA KILIMO KUONGEZA USHIRIKI WA VIJANA WENGI ZAIDI KATIKA KILIMO


*************

Naibu Waziri wa Kilimo Mh Anthony Mavunde ameweka bayana mkakati wa serikali katika kuwafanya Vijana wengi zaidi kushiriki katika sekta ya Kilimo ambapo amesema kwamba moja kati ya mkakati ni upatikanaji wa ardhi itayowekewa miundombinu rafiki ili kurahisisha shughuli ya kilimo.

Naibu Waziri Mavunde ameyasema hayo jana katika hafla fupi ya kuwaaga Vijana 16 wanaofanya shughuli za kilimo wanaokwenda katika maonesho ya Biashara na Kilimo nchini Uturuki na Dubai kwa ufadhili wa serikali chini ya uratibu wa Taasisi ya Chama cha Wafanyabiashara Wanawake (TABWA) ambapo alitumia fursa hiyo kuwataka Vijana waliopata nafasi kushiriki maonesho hayo kuitangaza vyema Tanzania na kuhakikisha safari hiyo inaleta mchango chanya katika maendeleo ya kilimo nchini.

“Kupitia Program hii ya TOBOA NA KILIMO vijana watapata fursa ya kushiriki kwenye kilimo kwa serikali kuweka mazingira wezeshi ikiwemo upatikanaji wa ardhi,mitaji,miundombinu ya umwagiliaji,upatikanaji wa pembejeo na mwisho kuwatafutia masoko ya mazao yao.

Tutatengeneza maeneo ya kilimo (agricultural parks),maeneo hayo yatafanyiwa vipimo (soil analysis )na upembuzi sambamba na miundombinu ya maji na barabara”Alisema Mavunde

Akizungumza Katika hafla hiyo,Afisa Biashara wa Ubalozi wa Uturuki nchini Tanzania Ndg.Onur Bilgen amewataka vijana hao kujifunza teknolojia sahihi ya kilimo wakiwa chini Uturuki ili warudishe ujuzi huo nchini kwa maendeleo ya kilimo.

Akishukuru kwa niaba,Mkurugenzi Mtendaji wa TABWA Bi. Noreen Mawala ameishukuru serikali kwa kuona umuhimu wa kushirikiana na Taasisi yake kugharamia safari ya Vijana hao kushiriki katika maonesho hayo kwa lengo la kupata ujuzi na masoko ya bidhaa zao.

Post a Comment

0 Comments