Ticker

6/recent/ticker-posts

ZINGATIENI MIONGOZO KATIKA KUFANYA TATHMINI ZA ULEMAVU

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, MOROGORO

MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando ametoa ushuhuda jinsi alivyofaidika na Mafao ya Fidia kutoka Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) wakati alipopata ajali akiwa kazini, Agosti 2021.

Ushuhuda huo aliutoa mjini Morogoro Machi 18, 2022 wakati akizungumza na Madaktari mwishoni mwa Mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kufanya Tathmini ya Ulemavu na Magonjwa yatokanayo na Kazi, yaliyoandaliwa na WCF.

Alisema suala la fidia ni muhimu sana kazini kwani ajira yoyote inaweza kubeba hatari fulani fulani na Mfanyakazi anapokuwa na uhakika wa kufidiwa pindi anapopata ajali au ugonjwa unaohusiana na Kazi anayoifanya basi morali ya kujituma katika kazi huongezeka.

“Niwapongeze WCF kwa kazi nzuri wanayofanya, mimi mwenyewe ni shuhuda mwezi Agosti nilipata ajali wakati nikiwa kazini na nilipofikishwa pale Muhimbili niliwakuta WCF wako pale”. Alisema Mhe. Msando.

Akifafanua zaidi alisema alilipwa gharama alizotumia kabla ya matibabu kukamilika, pia alilipwa wakati akiwa nje ya Ofisi na pia alilipwa Fidia ya madhara aliyoyapata.

Akizungumzia kuhusu mafunzo hayo, Mhe. Msando alisema “Lengo la mafunzo haya ya siku tano ni kuwaongezea ujuzi ambao hamkuwa nao hapo kabla.

“Ninyi kama watathmini lazima mtambue kwamba ni watoa haki na kwa namna mojawapo mnaamua hatma ya maisha ya huyo mfanyakazi baada ya kupata ulemavu kwahiyo ninyi mnawajibika kwenye maamuzi ya mtu huyu ameathirika kwa kiasi gani kwa kuzingatia miongozo ya tathmini na mnatoa haki kwa pande mbili yaani Mfuko na muathirika.” Alifafanua. Ninyi ni watoa haki zaidi ya kutoa huduma za kidaktari, kwahiyo nyie ndio mnafanya maamuzi yanayogusa hatma ya maisha ya mtu baada ya kuathirika, na hali hiyo ni ya pande zote mbili, Mfanyakazi aliyepatwa na majanga lakini na WCF pia, alibainisha.

“tunawategemea ninyi mkatoe Elimu kwa wale mnaowafanyia Tathmini kwani wengine uelewa wao bado ni mdogo.

“Kuna mtu anaweza kuhoji kwanini mimi nimelipwa fidia kiasi hiki wakati nimekatika kiungo, kwa hivyo ni vema ukamuelimisha vizuri. Kwa upande wake Mkurugenzi wa huduma za Tathmini WCF, Dkt.Abdulsalaam Omar amesema Mafunzo hayo yamewahusisha Madaktari kutoka Mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani, Dar es salaam na Morogoro. “Mafunzo kama haya yameanza muda mrefu toka Mfuko ulipoanzishwa mwaka 2015, kwani Madaktari ni kiungo Muhimu sana kwetu, hawa ni daraja kati ya Mfuko na Wafanyakazi watakaopatwa na majanga.” Alisema.

“Tunataka Tathmini za ulemavu zinazo zingatia viwango na ziwe sahihi zikifanyika sehemu yoyote nchini, Mfanyakazi aliyepata ajali Mtwara na akapata Ulemavu wa aina fulani basi aina Ile Ile ya Ulemavu ikifanyiwa Tathmini Kigoma zile Tathmini tunataraji ziwe sawa sawa na ndio lengo hasa la kutoa Mafunzo haya.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake, Dkt. Meekson Jackson Mambo kutoka Hospitali ya Bochi jijini Dar es Salaam aliishukuru WCF kwa kuwapatia mafunzo hayo kwani yamekuwa na manufaa makubwa kwao.

“Tunaahidi kuwa mabalozi wazuri huko tuendako ili kuiwezesha WCF kutimiza malengo ya kuanzishwa kwake.” Alisema.


MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando alipokuwa akizungumza na Madaktari na Watoa Huduma za Afya wakati akifunga Mafunzo ya Tathmini za Ulemavu na Magonjwa yatokanayo na Kazi mjini Morogoro Machi 18, 2022.
Baadhi ya washiriki wakionyesha stika watakazobandika kwenye ofisi zao kama alama ya watoa huduma za Tathmini.




Mkurugenzi wa Huduma za Tiba na Tathmini Dkt.Abdulsalaam Omar akielezea lengo la mafunzo hayo.
Dkt. Meekson Jackson Mambo, akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Elimu kwa Umma, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bi. Laura Kunenge (kulia) akimkabidhi stika mmoja wa washiriki. Stika hizo walikabidhiwa washiriki wote ili wakazibandike kwenye hospitali zao zikionyesha huduma ya Tathmini za Ulemavu na Magonjwa yatokanayo na Kazi zinapatikana mahali hapo.




Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo, Mgongo na Mishipa ya Fahamu, Dkt. Robert Mhina, ambaye ni Mwenyekiti wa Kikosi Kazi cha Utoaji Mafunzo hayo, akishirikiana na Dkt. Pascal Magessa kutoka WCF, wakionyesha kwa vitendo jinsi ya kufanya Tathmini ya ulemavu wa Miguu na Nyonga (Lower Limb)




Baadhi ya washiriki




Dkt.Abdulsalaam Omar (kulia) akishiriki katika majadiliano ya vikundi.
Dkt. Pascal Magessa (kushoto), akishiriki kwenye majadiliano ya vikundi




Dkt. Matilda Rusibamaila kutoka WCF, akifuatilia majadiliano ya vikundi.






Dkt.Damian Elias akifuatilia majadiliano ya vikundi.






MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msando, akimkabidhi Cheti cha ushiriki, mmoja wa Madaktari.

Post a Comment

0 Comments