Ticker

6/recent/ticker-posts

DKT. ABBAS KUZINDUA TAMASHA LA 13 LA UTAMADUNI WA MUZIKI WA CIGOGO



************

Na Mwandishi Wetu, Chamwino.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo,Dkt.Hassan Abas, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Tamasha la 13 la utamaduni wa muziki na ngoma za Wagogo maarufu kama Cigogo Music festival, litakalofanyika kwa siku mbili Julai 23-24, Kijiji cha Chamwino Ikulu, Mkoani Dodoma.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sanaa Chamwino (Chamwino Arts Center), Frank Mgimwa, alisema kuwa, wanatarajia kuwa na ugeni huo wa Katibu Mkuu, Dkt Abas ambaye atamwakilisha Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Mohammed Mchengerwa.

"Maandalizi yote ya tamasha yamekamilika na kwa Uzinduzi utafanywa na Katibu Mkuu Dkt Abas, hapa Chamwino.

Pia wadau wa muziki na Sanaa wa ndani na nje pia wataudhuria tamasha hili." Alisema Mgimwa.

Mgimwa alibainisha kuwa, Vikundi 32 vinatarajiwa kuonesha burudani mbalimbali kwa siku mbili ya tamasha hilo,

"Vikundi 32, kati ya hivyo vikundi 27 vinatoka Mkoa wa Dodoma na vikundi vitano vinatoka nje ya Mkoa wa Dodoma.

Vipo kutoka Mikoa ya Singida, Iringa, Njombe, Dar es Salaam na Morogoro."Alisema.

Aidha, Mgimwa aliongeza kuwa, Tamasha hilo limekuwa na mafanikio mbalimbali ikiwemo mzunguko mkubwa wa fedha ndani ya kijiji cha Chamwino Ikulu pamoja na mkoa wa Dodoma kwa ujumla, kwani kila mwaka huleta wasanii zaidi ya 1000 na wasanii hao pamoja na wageni angalau 200 kila mwaka ambapo hutumia nyumba za kulala, vyakula na huduma za kibenki ndani ya Chamwino.

"Tamasha limezaa miradi mbalimbali ndani ya Chamwino ikiwemo na Maktaba ya kisasa ya Shule ya Sekondari ya Chamwino ambapo makataba hii imeunganishwa na mkonga wa Intaneti, ina kompyuta zipatazo 11, ina vifaa vya kisasa vya kujisomea (kindle)300 ina vitabu pamoja na shelves za vitabu,

Lakini pia, tamasha limeleta mradi wa ufadhili wa wanafunzi ambao wanafanya vizuri darasani na wanatoka katika kaya maskini mpaka sasa zaidi ya wanafunzi 30 wamefadhiliwa katika ngazi mbali mbali za Elimu kuanzia shule ya Sekondari mpaka Shahada za Uzamivu.

Na kuongeza, "Tamasha limekua chanzo cha kipato kwa makundi ambayo hua yanashiriki katika Tamasha.

Tamasha limekua chanzo cha Makundi mbalimbali kusafiri kwenda nchi mbalimbali ili kuonesha Utamaduni wa Mtanzania nchi kama India, Spain, Ujerumani, Poland na kwingineko." Alisema Mgimwa.

Katika kuhakikisha Vijana wanakuwa na dira, Mgimwa alisema kuwa, tamasha limekua sehemu ya vijana kuweza kujifunza na kubadilishana uzoefu kupitia miradi ya umoja wa Ulaya Erasmus+ ambapo vijana wamepata fursa za kwenda nchi mbali mbali na kubadilishana uzoefu na masuala ya Utamaduni.

Post a Comment

0 Comments