Ticker

6/recent/ticker-posts

NSSF YAFADHILI MFUMO WA TAARIFA ZA DIASPORA

Mkurugenzi wa Uthaminishaji, Takwimu na Usimamizi wa Hadhari wa NSSF, Ibrahim Maftah (kushoto) wakionyesha hati ya Makubaliano jijini Dar es Salaam, Leo na Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi James Bwana, baada ya kutiliana saini makubaliano ya ufadhili wa matengenezo ya mfumo wa kidigitali wa kutunza taarifa za Diaspora.


****************************

Na Magrethy Katengu

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, wameingia makubaliano kufadhili matengenezo ya mfumo wa kidigitali wa utunzaji wa taarifa za Watanzania Wanaoishi Nje ya Nchi (DIASPORA), kwa gharama ya Shilingi milioni 50.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi James Bwana aliishukuru Bodi ya NSSF na Menejimenti kwa kukubali kufadhili matengenezo ya mfumo huo, ambao utakapokamilika utawatambua, kuwasajili na kutunza taarifa za Diaspora wa Tanzania waliotapakaa duniani kote kupata huduma muhimu kutoka kwenye Nchi yao.

Mhe. Balozi Bwana amesema mfumo huo utakuwa chachu ya ushiriki wa Diaspora wa Kitanzania kidigitali katika shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwemo biashara, uchumi na uwekezaji licha ya umbali waliopo.

“Kwa niaba ya uongozi wa Wizara na Serikali kwa ujumla natoa shukurani za dhati kwa uongozi mzima wa NSSF wa kukubali kushirikiana nasi katika jambo hili muhimu kwa kutoa Shilingi milioni 50,” amesema.

Balozi Bwana amesema NSSF ni wadau muhimu wa kutoa huduma kwa Diaspora ambapo pamoja na huduma hizo kupitia dirisha la uwekezaji, Wizara imekuwa na mazungumzo na NSSF ili kuangalia namna wanavyoweza kushirikiana zaidi katika eneo la Uwekezaji kupitia uendelezaji wa viwanja vilivyopo katika Balozi za Tanzania nje ya nchi.

Balozi Mbwana amesema mfumo huo pia utawezesha kutekeleza kwa vitendo azma ya Serikali kuhamasisha taasisi mbalimbali nchini kuwekeza katika digitali ili kuongeza tija ya matumizi sahihi ya muda wanaohudumiwa na kupunguza urasimu, pamoja na kuiwezesha Wizara hiyo kwenda sambamba na dunia katika teknolojia.

Kwa upande wake, Ibrahim Maftah ambaye ni Mkurugenzi wa Uthaminishaji, Takwimu na Usimamizi wa Hadhari akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Masha Mshomba, amesema Mfuko unatambua na kuthamini mchango wa Diaspora katika kujenga uchumi wa Taifa.

Maftah amesema ushiriki wa NSSF katika kufanikisha kuanzishwa kwa mfumo huo unatokana na umuhimu wa suala lenyewe, lakini pia kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha Diaspora wanachangia kikamilifu maendeleo ya uchumi wa Taifa.

“Wakati wote NSSF imekuwa moja ya wadau muhimu katika shughuli na matukio mbalimbali ya Diaspora, hivyo kupitia mfumo huo ni fursa kwa Mfuko kutangaza fursa mbalimbali za miradi ya uwekezaji kama vile nyumba, viwanja, hoteli na huduma nyingine zinazotolewa na NSSF,” amesema.

Aliipongeza Wizara kwa kubuni wazo hilo la kuanzisha mfumo huo ambao utakuwa chachu ya mafanikio mbalimbali ya kuwaunganisha Watanzania waliopo nje ya nchi na fursa mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Mwakilishi wa Kitengo cha Diaspora Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Semeni Nandonde, amesema kupitia mfumo huo Serikali itaweza kufahamu idadi ya Diaspora, ujuzi walionao, elimu pamoja na kupata huduma maalum ambazo zitaandaliwa kwa ajili yao kama vile huduma za hifadhi ya jamii, benki, bima ya afya, uwekezaji, biashara na masoko.

Aidha Diaspora wote wameshauriwa kutambua kuwa Mfumo huo utawawezesha kupata huduma maalum zikiwemo za hifadhi ya jamii, uwekezaji, biashara na masoko

Post a Comment

0 Comments