Ticker

6/recent/ticker-posts

WATOTO 360,000 KUPEWA CHANJO KUJIKINGA NA UGONJWA YA POLIO MKOA WA SINGIDA

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Jerry Muro, akiwa amempakata mtoto Harry Nickoson wakati akipatiwa chanjo ya Polio wakati wa uzinduzi wa kampeni ya utoaji wa chanjo ya matone awamu ya tatu dhidi ya ugonjwa wa polio ambapo kimkoa uliofanyika katika Halamshauri ya Wilaya ya Ikungi mkoani Singida leo hii. Mhe. Muro alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba katika uzinduzi huo.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Jerry Muro, akikata utepe kuashia uzinduzi wa chanjo hiyo. Kutoka kushoto ni Afisa Elimu Msingi , Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Margaret Kapolesya ambaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo katika uzinduzi huo na kulia ni mama wa mtoto Harry Nickoson ambaye alipatiwa chanjo kwa niaba ya watoto wengine wakati akiwa amembeba mwanaye huyo.
Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Solomon Michaelakizungumza kwenye uzinduzi huo.
Afisa Elimu Msingi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Margaret Kapolesya, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo.
Mratibu wa Chanjo Mkoa wa Singida, Habibu Mwinory akitoa taarifa fupi kuhusu maandalizi ya chanjo hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Jerry Muro, akiwa amempakata mtoto Giann Kapian Madondola wakati akipatiwa chanjo ya Polio wakati wa uzinduzi wa kampeni ya utoaji wa chanjo ya matone awamu ya tatu dhidi ya ugonjwa wa polio kwa nyumba kwa nyumba. Kulia anayeshuhudia tukio hilo ni Mama wa mtoto huyo, Zawadi Mlugu.
Waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali wakiwa tayari kuchukua taarifa hiyo.
Zulfa Ramadhani akiwa amempakata mtoto wake,Greyson Anatory akisubiri kupatiwa chanjo hiyo.
Wakina mama wakiwa wamewapakata watoto wao wakisubiri kupatiwa chanjo.
Uzinduzi wa chanjo hiyo awamu ya tatu ukifanyika.
Wakina mama wakisubiri watoto wao wapate chanjo.
Wakina mama wakiwa kwenye uzinduzi wa chanjo hiyo.
Uzinduzi wa chanjo ukiendelea.
Uzinduzi wa Chanjo ukiendelea.Kutoka kulia ni Afisa kutoka Idara ya chanjo Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Happy Saiguran na kushoto ni Jadili Muhanginonya kutoka katika ofisi hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Jerry Muro akiwa amembeba mtoto aliyepatiwa chanjo hiyo katika uzinduzi huo.
Picha ya pamoja baada ya kufanyika uzinduzi huo.


************************

Na Dotto Mwaibale, IKUNGI

MKOA wa Singida unatarajia kutoa chanjo ya matone dhidi ya ugonjwa wa polio kwa watoto 363,315 katika kampeni ya awamu ya tatu wenye umri chini ya miaka mitano ili kujikinga na maradhi hayo.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Jerry Muro, alisema hayo leo katika uzinduzi wa kampeni ya utoaji wa chanjo ya matone dhidi ya ugonjwa wa polio kimkoa uliofanyika katika Halamshauri ya Wilaya ya Ikungi.

Serukamba alisema katika chanjo hiyo ambayo imeanza kutolewa leo Septemba Mosi itafanyika hadi 4 Septemba na kuagiza kila halmashauri ya mkoa huu kuhakikisha inawafikia walengwa wake wa chanjo ya matone dhidi ya ugonjwa wa Polio.

Alitoa mchanganuo kuwa katika kampeni hiyo ambayo itakuwa ni ya awamu ya tatu, wilaya ya Iramba inatarajiwa kuwafikia watoto 56,360 ,Wilaya ya Singida vijijini watoto 58,197, Manyoni 45,416 Manispaa ya Singida watoto 39,841, Wilaya ya Ikungi 77,638, Wilaya ya Mkalama watoto 51,658 na Itigi watoto 34,205.

Alisema kauli mbiu ya kampeni hiyo ni "Kila tone la chanjo ya Polio litawekwa Tanzania salama dhidi ya Ugonjwa wa kupooza" ambapo kupitia kampeni hiyo inategemewa watoto wote wenye umri wa chini ya miaka mitano watapatiwa.

Serukalmba alisema kuanza kutolewa kwa chanjo hiyo kunafuatia Shirika la Afya Duniani (WHO) ilipofika 17 Februari 2022 lilitoa taarifa ya uwepo wa mlipuko wa ugonjwa wa Polio (Wild polio Virus) nchini Malawi ambapo hadi sasa Malawi imeripoti visa viwili toka mlipuko huu utangazwe mwezi huo.

Aidha, nchi ya Msumbiji imeripoti visa vinne (4) ambapo kisa cha kwanza nchini humo kiliripotiwa mwezi Mei, 2022.

Alisema kufuatia kuonekana kwa ugonjwa huo wa Polio katika Ukanda wa Kusini mwa Afrika, WHO ilitoa tamko kuwa Ugonjwa wa Polio ni janga la Kimataifa (Public Health Emergence of International Concern).

Mkuu huyo wa mkoa alisema tamko hilo la WHO lilikuwa na maana kuwa kugundulika kwa mtoto mmoja mwenye ugonjwa huu kuna uwezekano wa uwepo wa watoto zaidi ya mia mbili wenye maambukizi na uwezo wa kuambukiza watoto wengine na hata watu wazima ambao hawajapata chanjo.

"Shirika la Afya Duniani (WHO) linaelekeza kuwa unapotokea mlipuko au tishio la mlipuko wa ugonjwa wa Polio nchini, nchi husika na nchi jirani zinapaswa kufanya Kampeni ya kutoa chanjo kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano (5) kwa awamu nne mfululizo ili kila mtoto aweze kupata kinga kamili," alisema Serukamba.

Aliongeza kuwa kufuatia mlipuko wa ugonjwa huu katika nchi za Malawi na Msumbiji, na kwa kuzingatia ukaribu wa kijiografia na mwingiliano wa watu kati ya Tanzania, Malawi na Msumbiji kwa shughuli za kiuchumi na kijamii, kuna uwezekano mkubwa wa maambukizi ya Ugonjwa wa Polio kusambaa na kuingia nchini.

Serukamba alisema ili kuweza kudhibiti ugonjwa huu usiingie nchini na kwa kuzingatia Mwongozo wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wadau wa huduma za chanjo nchini inatekeleza Kampeni ya kutoa Chanjo ya Polio kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

"Awamu ya kwanza ya kampeni ilifanyika 24 hadi 27 Machi 2022 na ilitekelezwa katika mikoa minne inayopakana jirani na nchi ya Malawi ambayo ni Mbeya, Songwe, Njombe na Ruvuma. Kampeni hii ililenga kuwafikia watoto 975,839 wenye umri chini ya miaka mitano, na kufanikiwa kuwafikia watoto 1,130,261 sawa na asilimia 115 ya walengwa wote," alisema Serukamba.

Alisema katika awamu ya pili ya Kampeni hii ilifanyika nchi nzima kuanzia tarehe 18 hadi 21 Mei, 2022 ikilenga kuwafikia Watoto 290, 485 wenye umri chini ya miaka mitano, na kufanikiwa kuwafikia watoto 363,315 sawa na asilimia 125 ya walengwa wote ndani ya Mkoa wa Singida.

"Mkoa wa Singida unawapongeza na kuwashukuru Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Wataalamu wa Afya, Mashirika ya Kitaifa na Kimataifa, Vyombo vya Habari na wananchi kwa kufanikisha vyema utekelezaji wa Kampeni hii kwa awamu ya kwanza na ya pili," alisema.

Post a Comment

0 Comments