Ticker

6/recent/ticker-posts

KAMATI KUU YAMPONGEZA RAIS SAMIA

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM ambae ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akiongoza Kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM kilichofanyika tarehe 28 Oktoba, 2022 Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa pia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi (kulia) akifuatana Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Adalla Juma Sadala (kushoto)alipowasili Chamwino kushiriki Kikao cha Kamati Kuu ya CCM Taifa kilichofanyika leo (katikati) Naibu Katibu Mkuu CCM Bara.[Picha na Ikulu] 28/10/2022. Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Taifa pia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Mama Samia Suluhu Hassan (katikati) mara akiingia katika Ukumbi wa Kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichofanyika leo Chamwino Mkoani Dodoma.[Picha na Ikulu] 28/10/2022. Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa pia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi akisalimiana na Makamo wa Mwenyekiti wa CCM Bara Mhe.Abrahaman Kinana(katikati) kabla ya kuanza Kikao cha Kamati Kuu ya CCM Taifa kilichofanyika leo katika Ukumbi wa Chamwino Mkoani Dodoma(kulia) Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dk.Philip Mpango.[Picha na Ikulu] 28/10/2022.

Wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM wakiteta katika ukumbi wa Mikutano wa Chamwino Mkoani Dodoma kabla ya kuanza Kikao hicho leo (kulia) Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Tulia Acson na Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibae Mhe.Zubeir Ali Maulid(kushoto).[Picha na Ikulu] 28/10/2022.

*******************

*Ni kuhusu utayari wake wa kuimarisha demokrasia, kikosi kazi chatajwa kuwa kielelezo

*Pia yampongeza Rais Dk. Hussein Mwinyi kwa kuendelea kuimarisha uhusiano wa kisiasa Z'bar


Na MWANDISHI WETU

KAMATI Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imefurahishwa na kumpongeza Mwenyekiti wa CCM, Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuonesha kwa vitendo nia yake ya kuimarisha demokrasia.

Pongezi hizo za Kamati Kuu zinatokana na hatua ya Rais Samia kupokea ripoti ya kikosi kazi alichokiunda kuratibu maoni na mapendekezo ya wadau mbalimbali juu ya mchakato wa mustakabali wa taifa katika uendeshaji wa siasa.

Hayo yameelezwa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka kupitia taarifa yake kwa umma kuhusu kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichoketi leo Oktoba 28, 2022 Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma na kuongozwa na Mwenyekiti wa CCM, Rais Samia.

"Pamoja na mambo mengine Kamati Kuu imempongeza kwa dhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ndugu Samia Suluhu Hassan kwa hatua ya kupokea ripoti ya kikosi kazi alichokiunda kuratibu maoni na mapendekezo ya wadau mbalimbali juu ya mchakato wa mustakabali wa taifa letu katika uendeshaji wa siasa.

"Hatua hiyo kubwa na ya kupigiwa mfano, tangu alipoingia madarakani Ndugu Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele katika kusimamia utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM 2020-2025, kuimarisha demokrasia ya vyama vingi vya siasa nchini na ujenzi wa maridhiano ya kitaifa ili kuliwezesha taifa letu kuendelea kuwa lenye utulivu wa kisiasa, umoja na amani kwa maendeleo endelevu," amesema Shaka katika taarifa hiyo.

RAIS MWINYI PIA APONGEZWA

Aidha, Shaka amesema Kamati Kuu pia imempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi kwa hatua yake ya kuendelea kuimarisha mahusiano ya kisiasa visiwani Zanzibar ambapo ameunda kikosi kazi cha kuratibu maoni kwa upande wa mambo maalum yanayohusu Zanzibar na kinaendelea vyema na majukumu yake hatua ambayo itaimarisha demokrasia, umoja na mshikamano.

Katika hatua nyingine Kamati Kuu imepokea taarifa ya awali ya maandalizi ya Mkutano Mkuu wa kumi (10) wa CCM Taifa unaotarajiwa kufanyika mwezi Disemba, 2022.

Shaka amesema Kamati Kuu imeridhishwa na hatua mbalimbali za maandalizi ya Mkutano Mkuu huo wa kawaida utakaofanyika kwa mujibu wa Katiba ya CCM ya mwaka 1977 toleo la mwaka 2022 Ibara ya 99(3),

“Mkutano Mkuu wa CCM wa Taifa utafanya mikutano yake ya kawaida mara tatu katika kipindi cha miaka mitano. Mikutano miwili kati ya hiyo itakuwa ya uchaguzi na mmoja utakuwa wa kazi. Kalenda ya vikao vya Chama itaonesha ni lini mikutano mitatu hiyo itafanyika. Lakini mkutano usiokuwa wa kawaida unaweza kufanyika wakati wowote ukiitishwa na Mwenyekiti wa CCM au ukiombwa na theluthi mbili ya wajumbe wote wa Halmashauri Kuu ya CCM ya Taifa.” amesema Shaka akinuku kifungu cha Katiba ya CCM.

Post a Comment

0 Comments