Ticker

6/recent/ticker-posts

SAGINI AIPONGEZA URA SACCOS KWA KUTOA ZAIDI YA BIL.394 KWA WANACHAMA WAKE

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe.Jumanne Sagini akizungumza na wanachama wa Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo cha Usalama wa Raia (URA SACCOS) wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 14 wa Ura Saccos kwa mwaka 2022 uliofanyika Jijini Mwanza.Mrajis Msaidizi wa Vyama vya fedha kutoka tume ya Maendeleo ya Ushirika,Bw.Josephat Kisamalale akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 14 wa Ura Saccos kwa mwaka 2022 uliofanyika Jijini Mwanza.
Mwenyekiti wa Ura Saccos Bw.Benedict Wakulyamba akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 14 wa Ura Saccos kwa mwaka 2022 uliofanyika Jijini Mwanza.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe.Jumanne Sagini akipata picha ya pamoja na wanachama wa Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo cha Usalama wa Raia (URA SACCOS) wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 14 wa Ura Saccos kwa mwaka 2022 uliofanyika Jijini Mwanza.


***********


Na Sheila Katikula,Mwanza

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe.Jumanne Sagini amekipongeza chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo cha Usalama wa Raia (URA SACCOS) kwa kutoa zaidi ya Sh Bilioni 394 kwa wanachama wake ambapo asilimia 75 ya mkopo huo ulielekezwa katika ujenzi wa nyumba za makazi kwa wanufaika.

Hayo ameyasema leo oktoba 27 wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 14 wa Ura Saccos kwa mwaka 2022 uliofanyika Jijini Mwanza.

Amesema wanachama wa Ura Saccos walifanikiwa kutumia mikopo iliyotolewa kwa riba ya asilimia 75 kufanya ujenzi wa nyumba binafsi za wanachama hao.

Amesema kupitia ujenzi wa nyumba zinazofanywa na mkopo walioupata kutoka Ura Saccos wamefanikiwa kuongeza mzunguko wa fedha katika Pato la Taifa (GDP) hivyo kuwafanya wananchi kuendelea na shughuli zao ipasavyo.

Sagini alisema iwapo kutakuwa na usimamizi mzuri wa vyama vya ushirika kwa njia ya kimaadili nchi inaweza kupata maendeleo ya haraka kupitia sekta hiyo.

"Serikali inafuraha kuona watumishi wa umma wanakuwa na juhudi katika mipango ya maendeleo, jambo ambalo linawasaidia kuridhika na kuweza kukabiliana na changamoto za kujihusisha na vitendo vya rushwa hivyo polisi wote wajiunge na saccos yao," alisema Sagini.

Mwenyekiti wa Ura Saccos, Bw.Benedict Wakulyamba amesema wamefanikiwa kutoa mikopo yenye thamani ya sh Bilioni 394.5 sawa na asilimia 75 ambazo zilitumika katika ujenzi wa nyumba, huku huduma nyingine za mtu mmoja mmoja zikitolewa kwa wanachama wagonjwa, huduma ya vifo kwa wanachama na wategemezi wao, fidia kwa majanga dhidi ya wanachama.

Amesema saccos hiyo ilianza mwaka 2006 ikiwa na wanachama 4300 huku wakati huo ikiwa na hisa ya sh 17,026,693 na sasa wana hisa ya sh 8,421,327,680 na wanachama 46,024 kutoka pande zote za nchi.

Wakulyamba amesema mwaka 2021 walitoa gawio la fedha taslimu sh 1,082,539,598 na walitoa akiba ya sh 3,357,065,139 waliwezesha sh 415,000,000 kwa hospitali, zahanati na vituo vya afya zinazomilikiwa na polisi nchini.

Pia aliipongeza serikali kwa kuimalisha mifumo na kusimamia, kuongeza mishahara na kupandisha vyeo kwa watumishi wa umma.

Amesema mikopo iliyotolewa ni juhudi za serikali za kuboresha maslahi ya watumishi wa umma.

Naye Mrajis Msaidizi wa Vyama vya fedha kutoka tume ya Maendeleo ya Ushirika nchini, Bw.Josephat Kisamalale amewapongeza polisi kwa kujiunga na saccos hiyo na kupelekea kuwa na wanachama wengi tofauti na saccos nyingine nchini.

Amesema kuna umuhimu wa kuanzishwa kwa Saccos kwani inasaidia serikali katika utoaji wa fedha kwa jamii.

Post a Comment

0 Comments