Ticker

6/recent/ticker-posts

RAIS SAMIA AMSHIKA MKONO KIJANA ALIYEONGOZA UOKOAJI

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akimpongeza na kumfariji kijana Jackson Majaliwa kwa ushujaa wake wa kuwahi katika eneo ilipotokea ajali ya ndege ya Shirika la Precision na kuwaokoa abiria waliokuwa wameshindwa kutoka ndani ya ndege hiyo. Maombolezo ya kuaga miili ya watu wa ajali hiyo yamefanyika katika uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba Mkoani Kagera 7/11/2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na waombolezaji waliojitokeza kuaga miili ya watu waliopata ajali katika ndege ya shirika la Precision, iliyotokea Novemba 5, 2022. Maombolezo hayo yamefanyika katika uwanja wa Kaitaba Bukoba Mkoani Kagera Jumatatu 7/11/2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) Ndege ya Shirika la Precision iliyopata ajali Novemba 6, 2022 ikiwa pembezoni mwa uwanja wa ndege wa Bukoba baada ya kuvutwa kutoka eneo la ajali. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akitoa pole kwa ndugu wa Marehemu waliojitokeza katika uwanja wa Kaitaba yalipofanyika maombolezo ya kitaifa ya wahanga wa ajali ya ndege ya shirika la Precision, Ajali hiyo ilitokea Novemba 5, 2022. Maombolezo hayo yamefanyika katika uwanja wa Kaitaba - Bukoba Mkoani Kagera Jumatatu 7/11/2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akitoa salamu za mwisho kwa miili ya watu waliopata ajali ya ndege ya shirika la Precision , iliyotokea Novemba 5, 2022. Maombolezo hayo yamefanyika katika uwanja wa Kaitaba Bukoba Mkoani Kagera Jumatatu 7/11/2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Miili ya marehemu waliofariki katika ajali ya ndege ya Shirika la Precision iliyotokea Novemba 5, 2022, ikiwa imewekwa katika eneo maalum kwenye uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba Mkoani Kagera kwa ajili ya kuagwa na kukabidhiwa kwa ndugu wa marehemu katika maombolezo yaliyofanyika kweye uwanja huo Jumatatu 7/11/2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

************************

RAIS Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameagiza kijana Majaliwa Jackson aliyeona ndege ikianguka na kuamua kwenda kutoa msaada wa uokoaji akabidhiwe kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na aingizwe katika Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ili apate mafunzo zaidi.

Hayo yamesemwa leo (Jumatatu, Novemba 7, 2022) na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati akiongoza wananchi kuaga miili ya watu 19 waliofariki katika ajali ya ndege ya shirika la ndege la Precision katika uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.

Ajali ya ndege hiyo aina ya ATR 42-500 yenye namba za usajili 5H-PWF iliyotokea jana asubuhi wakati ikijaribu kutua katika kiwanja cha ndege cha Bukoba ikiwa na watu 43 wakiwemo abiria 39, marubani wawili na wahudumu wawili.

Amesema kwamba taarifa za uokoaji zinaonesha kuwa watu waliookolewa ni 24 wakiwemo abiria 22 na wahudumu wa ndege wawili na waliopoteza maisha ni watu 19 wakiwemo abiria 17 na marubani wawili.

Pia, Waziri Mkuu amesema Rais Mheshimiwa Samia ameelekeza mazishi ya wahanga wote yatagharimiwa na Serikali, hivyo, amewaelekeza wakuu wa Mikoa katika maeneo husika wasimamie kikamilifu shughuli hiyo.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Kamati za Usimamizi wa Maafa katika ngazi ya Mkoa na Halmashauri ambazo Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya ndio wenyeviti zitaendelea kuimarishwa ili ziweze kuchukua hatua za haraka maafa yanapotokea.

Waziri Mkuu amesema kwa niaba ya Serikali ameendelea kuwapa pole wafiwa wote, ndugu, jamaa na marafiki na anawatakia safari njema na maziko mema kwa wale wanaosafiri kwenda mbali na maeneo hayo ya Bukoba.

Awali, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa alitumia fursa hiyo kuwaondoa hofu Watanzania kuwa waendelee kutumia usafiri wa anga kwa kuwa mamlaka husika zipo na zinasimamia na kuchukua hatua stahiki ya kuhakikisha uwepo wa usalama wa anga kwa ajili ya safari za ndani ya nchi.

Post a Comment

0 Comments