Ticker

6/recent/ticker-posts

WATUMISHI 21 TAASISI ZA UMMA KUSIMAMISHWA KAZI KUPISHA UCHUNGUZI.





*************************

Na Hamida Kamchalla, TANGA.


WATUMISHI 21 wa taasisi za umma wamesimamishwa kazi kupisha uchunguzi baada ya taarifa ya kamati ya uchunguzi kukamilisha kazi yake.

Akitoa maagizo ya kukamatwa watumishi hao, mkuu wa Mkoa wa Tanga Omari Mgumba amesema serikali ya sasa haiwezi kumuonea mtu yoyoyte bali inaenda na mienendo ya haki kwa wote na bila kumpendelea mtu.


Mgumba aliunda kamati ya uchunguzi juu ya suala la kuungua kwa ghala la kuhifadhia mali za magendo zinazokamatwa na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) Mkoa wa Tanga.


Pamoja na kuwasimamisha watumishi, pia aliagiza jeshi la polisi na TAKUKURU kuwafuatilia na kuwakamata wafanyabiashara wawili na mvuvi mmoja ambao wametuhumiwa katika tukio hilo.


"Kuna makosa mengine yakifanyika sio lazima kusubiria jeshi la polisi au TAKUKURU, hii ni ya kiikamati hivyo hawa watumishi wote waliopatikana na tuhuma hizi wanatakiwavkusimama kazi na kupisha uchunguzi wa tuhuma zao,


"Na ninyi Maofisa wa TRA na TPA mjitathini kwa nafasi zenu, lakini pia jeshi la polisi na TAKUKURU muwasake wafanyabiashara wawili ambao ni mtu na baba yake waliohusika katika tukio hili popote walipo muwakamate pamoja ha huyo mvuvi mmoja" amesisitiza.


Aidha amesema orodha ya watumishi hao katika taasisi zao na kwamba TRA wapo 7, TPA wapo 6 na Suma JKT wapo 7 lakini pia yupo mtumishi mmoja wa Mamlaka ya Viwango (TBS) ambaye alijihusisha na uchukuaji wa sampuli za kupima viwango ambayo inazidi kiwango cha kinachohitajika.


Watumishi kutoka Bandari ni Mkuu wa Usalama wa Bandari Fortunatus Sandaria,msaidizi wake Aliko Mwakipagala,Mlinzi Peter Mwankina, Msaidizi wake Issa Haruna,Jumes Kyaomoka na mlinzi Mwandamizi Suzan Kanyika.


Kwa upande wa watumishi wa TRA ni David Kisanga ambaye ni Afisa Forodha, Sophia Mwezimpya ambaye ni Afisa Forodha Daraja la pili, Nasoro Kupaza Meneja Msaidizi Forodha, Iddi Kimaro ambaye ni Afisa Forodha Mfawidhi, Hemedi Kavumo na Lameck Lima ambao wote ni Afisa Forodha akiwemo Anderson Mbuyabuye ambaye ni Afisa Forodha Msaidizi.



Hata hivyo amewataja kwa upande wa Suma JKT Bandarini ni Mwalimu Lupa Mwinyiwanga ambaye alikuwa ni kuli, Mussa Zayumba ambaye ni mlinzi wa geti la supply, Dickson Kanoni ambaye ni Mlinzi,


Zacharia Wilson ambaye ni msimamizi wa ulinzi Suma JkT Bandarini, David Kisaka ambaye ni Kibarua, Mashaka Mshihiri ambaye ni kuli na Magawa Kombo na Isumila Matulanga ambaye ni mtumishi wa TBS Tanga.


"Watuhumiwa wengine ni mfanyabiashara wa mzigo uliokamatwa Abdallah Ally maarufu kama Balozi akiwa na mwanae Siyahi Lukuni ikiwemo mvuvi mmoja Salim Ally, ambaye alikula njama ya kuhujumu"


Naye mwenyekiti wa kamati hiyo ya uchunguzi Sebastian Masanja ambaye amemkaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga Pili Mnyema alisema kamati inashauri kwamba TAKUKURU na jeshi la polisi waendelee na uchunguzi zaidi ili wahusika waweze kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.


"Aidha hatua za kinidhamu zichukuliwe kwa watumishi wote watakaobainika kuhusika katika uondoshwaji wa mizigo na uchomaji wa ghala, matarajio ya kamati ni kuwa kukamilika kwa uchunguzi huu ndio mwanzo wa hatua nyingine kuchukuliwa.

"Ili kusaidia wigo wa mapato kuongezeka katika Mkoa wetu endapo mapendekezo ya kamati yatazingatiwa na kufanyiwa kazi ipadavyo" amesema Masanja.

Post a Comment

0 Comments