Ticker

6/recent/ticker-posts

HOSPITALI TUMBI KUANZA KUCHUJA DAMU KWA WAGONJWA WA FIGO DESEMBA 15,2022


Daktari Bingwa wa huduma za ndani katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Tumbi wilayani Kibaha Mkoani Pwani Dk.Adam Gembe ambaye pia ni Msimamizi wa Kitengo cha huduma za uchujaji damu kwa wagonjwa figo akitoa maelezo ya vifaa walivyopokea kutoka Bohari ya Dawa(MSD) vikiwemo mashine za kuchuja damu kwa wagonjwa hao.

Wahandisi wa Bohari ya Dawa(MSD) wakiendelea na usimikaji wa mitambo ya mashine za kuchuja damu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tumbi.

Baadhi ya mashine za kuchuja damu kwa wagonjwa wa figo vikiwa tayari vimefungwa kwenye wodi ya wagonjwa hao katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tumbi ambapo imeelezwa huduma zinatarajiwa kuanza kutolewa katikati ya Desemba mwaka huu.

Ofisa Huduma kwa Wateja Kanda ya Dar es Salaam wa MSD ambaye pia ni Mfamasia Diana Kimario akitoa maelezo kuhusu huduma zinazotolewa na MSD katika hospitali hiyo.

************************

Mwandishi Wetu, Kibaha

HOSPITALI ya Rufaa Mkoa wa Tumbi iliyopo wilayani Kibaha mkoani Pwani, inatarajia kuanza kutoa huduma ya uchujaji wa damu kwa wagonjwa wa figo kuanzia katikati ya Desemba mwaka huu.

Hatua hiyo inatokana na maboresho makubwa yaliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan kwenye hospitali hiyo ikiwemo ya kuilekezea Bohari ya Dawa (MSD) kufunga vifaa tiba vya kisasa katika idara mbalimbali hususan idara ya wagonjwa wa figo ambako kumefungwa mashine 10 za kuchuja damu.

Akizungumza leo Desemba 5,2022 , Daktari Bingwa wa Huduma za Ndani katika Hospitali ya Rufaa mkoa wa Tumbi Dk.Adam Gembe ambaye pia anasimamia Kitengo cha huduma ya uchujaji damu amesema wamepata vifaa tiba vya kisasa kutoka Bohari ya Dawa na miongoni mwa vifaa hivyo kuna mashine 10 za kuchujaji damu kwa wagonjwa figo.



Amefafanua kati ya mashine hizo nane zitahudumia wagonjwa wasiokuwa na maambukizi ya VVU na mashine mbili ni kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa wenye VVU huku akisisitiza kwamba wataanza huduma hizo katikati ya Desemba na kwa sasa wako hatua za mwisho kusimika mitambo inayowezesha mashine kufanya kazi.

Amesema awali walikuwa wanawapatia rufaa wagonjwa kwenda Muhimbili kwasababu hakukuna na huduma hiyo kwenye hospitali hiyo jambo lililosababisha wagonjwa kutumia gharama kubwa ya matibabu.“Lakini sasa huduma za kibingwa zinapatikana hapa , katika idara zote ikiwemo idara ya wanawake, upasuaji mkubwa na upasuaji wa kawaida , idara ya masikio , koo. meno huduma zote zinapatikana,”

“Tunaishukuru MSD, kwa kutuletea mashine za kuchuja damu lakini tunaiomba kuendelea kuboresha huduma ya upatikanaji wa vitendanishi na vifaa tiba, vitakavyotusaidia kutoa huduma bila kukwama na kwa wakati,”amesema.

Kwa upande wa changamoto amesema zipo chache ikiwemo ya uhaba wa maji na tayari wameanza kuchukua hatua kwa kufikiria kuchimba kisima, kwani huduma ya uchujaji wa damu zinahitaji maji ya kutosha.Pia uwepo wa umeme wa uhakika ambao kupitia watalamu wa ndani wameanza kuangalia njia mbadala ya kuwa na umeme ukiwemo unaotokana na jua ili huduma hizo zisikwame.

Kwa upande wake Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Tumbi Dk.Erica Mrema, alisema kwa sasa wameboresha huduma za afya na miundombinu tofauti na ilivyokuwa zamani na lengo ni kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Pia tulikuwa hatuna vifaa tiba vya aina nyingi, tunamshukuru Rais Samia tumeweza kupata vifaa hivyo vya kisasa na kuboresha huduma ambazo hatukuwa nazo. Awali tulikuwa tunawapa rufaa wagonjwa kwenda Muhimbili, lakini sasa huduma za kibingwa zinapatikana hapa , katika idara zote ikiwemo idara ya wanawake, upasuaji mkubwa na upasuaji wa kawaida , idara ya masikio , koo. meno huduma zote zinapatikana.”

Amefafanua kwa sasa wanayo Kliniki ya Waraibu wa dawa za kulevya ,ICU ya watu wazima na watoto na CT Scan iliyotokana na fedha za UVIKO -19,“alisema.

Wakati huo huo Mfamasia wa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Tumbi Dk.Kilango Mchala amesema uwepo wa MSD ni muhimu katika maboresho sekta ya afya hususani katika kurahisisha utoaji huduma kwa wananchi huku akutoa mwito kwa bohari ya Dawa kuhakikisha kunakuwepo mazingira wezeshi ya upatikanaji wa dawa pamoja na vifaa tiba kwa wakati.

Kwa upande wake Ofisa Huduma kwa Wateja Kanda ya Dar es Salaam wa MSD, Diana Kimario alitoa rai kwa hospitali kujenga tamaduni za kuandika maombi ya dawa na vifaa tiba mapema kabla kuisha lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma stahiki.

Post a Comment

0 Comments