Ticker

6/recent/ticker-posts

TASAC YATUMIA MAONESHO YA BIASHARA,UWEKEZAJI NA FURSA KUTOA ELIMU KWA WANANCHI

SHIRIKA la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limetoa elimu kwa wananchi kuhusu namna linavyotekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria wakati wa maonesho ya Biashara, Uwekezaji na Fursa yaliyokuwa yakifanyika katika viwanja vya Mashujaa kuanzia tarehe 19 hadi 31 Machi, 2023 Mkoani Mtwara.
Akizungumza na vyombo ya habari wakati wa maonesho hayo Kaimu Afisa Mfawidhi wa Mkoa wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania Mkoa wa Mtwara,Joseph Myaka amesema kuwa katika kutekeleza majukumu yao shirika hilo limejikita katika kutoa elimu kwa wananchi kufahamu shirika hilo linavyotekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria.

Amesema kuwa licha ya majukumu makubwa waliyonayo waliamua kushiriki maonesho hayo ili kuwapa elimu wananchi kuhusu fursa za biashara zilizopo katika Sekta ya Usafiri kwa njia ya Maji sambamba na elimu kuhusu Usalama, Ulinzi na Utunzaji wa mazingira majini jukumu linalotekelezwa na Shirika hilo.

“TASAC tunashiriki maonesho haya ya Biashara Uwekezaji na Fursa mkoani Mtwara ili kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yanayotekezwa Kisheria. kama mdhibiti wa shughuli za usafiri kwa njia ya maji tunasimamia huduma zinazotolewa na Bandari, tunadhibiti na kusimamia ulinzi, usalama na utunzaji wa mazingira na kuratibu shughuli za uokoaji na utafutaji pale panapotokea dhoruba majini”.

“Pia tunatoa elimu kwa wananchi wa Mtwara na wadau wa usafiri kwa njia ya maji katika jukumu letu la Udhibiti wa Safari kwa njia ya Maji na udhibiti Usalama, Ulinzi na Utunzaji wa Mazingira majini, wanaweza kufanya shughuli zao kwa usalama na kupata maendeleo na kuongeza pato la Taifa.” Ameeleza Joseph.

Kwa mujibu wa Sheria, TASAC ina wajibu wa kusimamia kazi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuhimiza usimizi na shughuli za uwakala wa meli wenye ufanisi, kuhimiza shughuli za bandari na huduma za meli zenye ufanisi, kuhakikisha kunakuwepo usalama na ulinzi wa shehena, kuhimiza na kutunza mazingira, usalama na ulinzi wa bahari, maziwa na mito.

Maonesho hayo ya Biashara, Uwekezaji na Fursa ni maonesho ya Kwanza kufanyika Mkoani Mtwara yakiwa na lengo la kuwaleta pamoja wadau mbalimbali katika Sekta hiyo ili kubadilishana uzoefu wa kitaalamu na kujifunza biashara na uwekezaji wa kisasa pamoja na fursa zilizopo katika sekta hiyo na Mkoa wa Mtwara kwa ujumla.




Post a Comment

0 Comments