Ticker

6/recent/ticker-posts

WAKAZI 4115 KATA YA KITANGARI WILAYA YA NEWALA WAONDOKANA NA KERO YA MAJI,

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2023 Abdalla Shaibu Kaim kulia,akimtwisha ndoo ya maji mkazi wa kijiji cha Mandala wilayani Newala Farida Ismail baada ya kufungua mradi wa maji Mandala.
Kiongozi wa mbio za mwenge wa Uhuru mwaka 2023 Abdalla Shaibu Kaima kulia na Mbunge wa Jimbo la Newala vijijini Maimuna Mtanda kushoto,wakiondoa kitambaa kufungua rasmi mradi wa maji Mandala uliotekelezwa na wakala wa maji safi na usafi wa mazingira vijijini(Ruwasa)kwa gharama ya Sh.milioni 331.
Mkuu wa wilaya ya Newala Rajabu Kundya.akizungumza na wakazi wa kata ya Kitangari kabla ya Mwenge wa Uhuru kufungua rasmi mradi wa maji Mandala wilayani humo,kulia Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2023 Abdalla Shaib Kaim na kushoto meneja wa Ruwasa wilaya ya Newala Mhandisi Sadik Nsajigwa.

Mkimbiza Mwenge wa Uhuru Kitaifa Martin Mkanga kulia,akimsikiliza meneja wa wakala wa maji safi na usafi wa mazingira vijijini(Ruwasa) wa wilaya ya Newala mkoani Mtwara Mhandisi Sadik Nsajigwa kabla ya kiongozi wa mbio za Mwenge Abdalla Shaibu Kaim kufungua mradi wa maji Mandala.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Mwaka 2023 Abdalla Shaibu Kaimu akifungua koki baada ya kukagua ujenzi wa mradi wa maji Mandala Halmashauri ya wilaya Newala mkoani Mtwara.

Meneja wa Ruwasa wilayani Newala Sadik Nsajigwa aliyeshika fimbo,akimuonyesha Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaofa mwaka 2023 Abdalla Shaibu Kaim kushoto,mchoro wa mradi wa maji Mandala uliotekelezwa na Ruwasa kwa gharama ya zaidi ya Sh.milioni 331.

*************************

Na Muhidin Amri, Newala

SERIKALI imetumia zaidi ya Sh.milioni 331.4 kumaliza changamoto ya maji kwa wakazi wa vijiji vitano vyenye wakazi 4,115 katika kata ya Kitangari,Mtunguru na Muungano wilayani Newala.

Meneja wa Ruwasa wilayani Newala Mhandisi Sadik Nsajigwa ametaja vijiji vitavyonufaika na mradi huo ni Mandala,Namkonda,Mpotola,Mnali na Mkupete ambapo ameeleza kuwa mradi huo umefikia asilimia 100 ya utekelezaji wake na umeanza kutoa huduma.

Nsajigwa amesema,mradi wa maji Mandala ulianza kutekelezwa Mwezi Januari na umekamilika mwezi Mei 2022 na hadi sasa Mkandarasi amemaliza kazi zote alizopewa kwa mujibu wa mkataba.

Amesema,mradi huo umesaidia sana kuunganisha huduma ya maji kwa wananchi wa maeneo hayo ambao awali walilazimika kutumia maji ya visima vya asili na mabonde yaliyopo umbali wa kilomita 7 kutoka katika makazi yao.

Nsajigwa alitaja kazi zilizotekelezwa ni ulazaji wa mtandao wa bomba wenye urefu wa kilomita 25.2 na ujenzi wa vituo 16 vya kuchotea maji na vijiji vyote vilivyopitiwa na mradi huo vimeingizwa kwenye kamati ya maji iliyoboreshwa(CBWOS)-Umoja na mpaka sasa chombo hicho kimefanikiwa kukusanya jumla ya Sh.milioni 2,075,000 tangu kilipoanzishwa.

Nsajigwa alieleza kuwa,mradi huo umetekelezwa na Mkandarasi kampuni ya ULM Investmeng Co Ltd na kusimamia na Wakala wa maji safi na usafi wa mazingira vijijini(Ruwasa)umekamilika kwa asilimia 100.

Kwa upande wake Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2023 Abdalla Shaibu Kaim amesema, utekelezaji wa mradi huo ni moja ya mkakati wa serikali ya awamu ya sita kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi wa maeneo ya vijijini kwa asilimia 85 na maeneo ya mjini angalau kwa asilimia 95 ifikapo mwaka 2025.

Kaim,ameipongeza serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutambua changamoto za wananchi wanaoishi maeneo ya vijijini ikiwemo ya maji safi na salama na kuzipatia majawabu.

Amesema,hatua ya serikali kutoa fedha nyingi zilizowezesha kutekeleza mradi huo ni dhahiri imeonesha mapenzi makubwa na kutimiza ahadi yake ya kufikisha huduma ya maji karibu na wananchi chini ya kauli mbiu ya kumtua mama ndoo kichwani.

Ametoa wito kwa wakazi wa Mandala,kuhakikisha wanatunza na kulinda mradi huo na miundombinu yake sambamba na kutunza vyanzo vya maji ili miradi inayotekelezwa iweze kudumu kwa muda mrefu na ilete manufaa kwa watu wote.

Kiongozi huyo wa Mwenge kitaifa,amewapongeza wataalam wa Ruwasa ngazi ya wilaya na Mkoa wa Mtwara kwa kazi kubwa wanayofanya katika kusimamia na kutekeleza miradi ya maji kwa viwango na ubora wa hali ya juu.

Mkandarasi wa mradi huo kutoka kampuni ya ULM Investmeng Co Ltd
Mwanahamisi Ngalemwa ameishukuru Serikali ya awamu ya sita kuwapa kazi na kuwaamini wakandarasi wanawake katika kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo miradi ya maji.

Amesema,tangu serikali ya Dkt Samia iingie madarakani kumekuwa na mabadiliko makubwa kwa wakandarasi ambapo sasa wanapata kazi nyingi na malipo ya kazi zao yanafanyika kwa haraka tofauti na hapo awali.

Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Mandala,wameishukuru serikali kuwajengea mradi wa maji uliomaliza mateso ya kutembea umbali wa kilomita 7 hadi kijijini jirani cha Mitema kufuata maji kwa matumizi yao.

Wamesema,kabla ya kujengwa kwa mradi huo walitumia muda wao mwingi kutafata maji badala ya kujikita katika shughuli za maendeleo hali iliyosababisha umaskini mkubwa miongoni mwao.

Fatuma Lipapa alisema,ujenzi wa mradi wa maji Mandala umemaliza kero ya kuamka usiku wa manane kwenda kutafuta huduma ya maji mbali na makazi yao na kuishukuru Serikali kwa kukamilisha mradi huo.

Lipapa alisema,katika kijiji hicho changamoto kubwa ilikuwa kupata chanzo cha uhakika cha maji,hivyo walilazimika kutumia maji ya visima vya asili na wakati mwingine kutega maji ya mvua wakati wa masika.

Chimatola Natepa,ametoa ushauri kwa Ruwasa kujenga tenki lingine ambalo litasaidia kuzuia presha kubwa ya maji yanatoka kwenye chanzo kabla ya kufika kwa watumiaji hali inayosababisha kupasuka kwa mabomba mara kwa mara.

Post a Comment

0 Comments